• HABARI MPYA

    Thursday, April 12, 2018

    MROMANIA ACHUNGULIA MLANGO WA KUTOKEA AZAM FC, PLUIJM ANABISHA HODI CHAMAZI

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KOCHA Mromania, Aristica Cioaba hataongezewa mkataba kwa sababu Azam FC ina mpango wa kumchukua Mholanzi, Hans van der Pluijm.
    Pluijm ambaye kwa sasa anafundisha Singida United inasemekana tayari amekwishafikia makubaliano na uongozi wa Azam FC na wakati wowote anaweza kusaini mkataba kabla ya kutambulishwa.
    Azam FC imedhamiria kuachana na Cioaba baada ya timu kushindwa kutwaa taji lolote Tanzania Bara kwa msimu wa pili mfululizo sasa.
    Wakati Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inaelekea ukingoni, Azam FC imeachwa mbali na Simba na Azam FC katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu kiasi cha kukatisha tamaa kama inaweza kutwaa taji hilo.
    Azam FC itakuwa timu ya tatu kwa Hans van der Pluijm kufundisha Tanzania baada ya Yanga na Singida United 

    Azam FC inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ikiwa pointi 45 baada ya kucheza mechi 23, nyuma ya mabingwa watetezi, Yanga wenye pointi 47 za mechi 22 na Simba SC wenye pointi 52 za mechi 22 pia. 
    Wakati huo huo, tayari imetolewa mapema tu kwenye michuano ya Azam Sports Federation Cup (ASFC) katika hatua ya Robo Fainali ikifungwa kwa penalti 9-8 na Mtibwa Sugar ya Morogoro baada ya sare ya 0-0.
    Hayo ‘yamewafika kooni’ wamiliki na viongozi wa Azam FC na kwa pamoja wamesema ‘inatosha kwa Cioaba’ na sasa wanataka wajaribu kwa kocha wa zamani wa Yanga, Pluijm.
    Pluijm alikuja Tanzania mwaka 2014 na kujiunga na Yanga SC alikofanya kazi kwa msimu mmoja kabla ya kwenda Al Shoalah FC ya Saudi Arabia na kurejea Jangwani mwaka 2015 akafanya kazi Novemba 2016 alipohamia Singida United.
    Cioaba alijiunga na Azam FC Januari mwaka jana akichukua nafasi ya makocha Waspaniola, chini ya Zeben Hernandez Rodriguez na ameshinda taji moja moja tu, Kombe la Mapinduzi Januari mwaka huu. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MROMANIA ACHUNGULIA MLANGO WA KUTOKEA AZAM FC, PLUIJM ANABISHA HODI CHAMAZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top