• HABARI MPYA

    Thursday, April 26, 2018

    KUTINYU WA SINGIDA UNITED AFUNGIWA MECHI NA TATU NA FAINI JUU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI Mzimbabwe, Tafadzwa Kutinyu wa Singida United amefungiwa mechi tatu na kupigwa faini ya Sh. 500,000 kwa kufanya vitendo vyenye kuonyesha imani za ushirikina katika mechi namba 177 dhidi ya Mtibwa Sugar Aprili 6, 2018 kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida.
    Katika mchezo huo, Kutinyu alichukua taulo la kipa wa Mtibwa Sugar na kulirusha jukwaani kwa washabiki wa Singida United ambao waliondoka nalo. Adhabu dhidi yake imetolewa kwa mujibu wa Kanuni ya 37(7) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti wa Wachezaji.
    Singida United pia imepigwa faini ya Sh. 500,000 kwa kutumia mlango usio rasmi kuingia uwanjani katika mechi dhidi ya Yanga SC Aprili 11, 2018 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Tafadzwa Kutinyu (kushoto)  akiwa na kocha wake, Hans van der Pluijm

    Kitendo hicho ni ukiukaji wa Kanuni ya 14(14) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo, na adhabu dhidi ya klabu hiyo ni uzingativu wa Kanuni ya 14(49) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.
    Vilevile Bodi ya Ligi imepeleka malalamiko kwenye Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) dhidi ya Meneja wa Singida United, Ibrahim Mohamed kwa kuongoza vurugu za timu yake kulazimisha kuingia uwanjani kwa kutumia mlango usio rasmi.
    Nayo Mbao FC imepigwa faini ya Sh. 500,000 kutokana na mshabiki wake kuingia uwanjani na kuchukua glovu za akiba za kipa wa Lipuli zilizowekwa golini na kukimbia nazo, kitendo kinachoonyesha imani za kishirikina.
    Adhabu dhidi ya Mbao katika mechi hiyo iliyofanyika Aprili 6, 2018 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 42(1) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti wa Klabu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KUTINYU WA SINGIDA UNITED AFUNGIWA MECHI NA TATU NA FAINI JUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top