• HABARI MPYA

    Saturday, April 28, 2018

    YANGA SC WAREJEA DAR KIMYA KIMYA, WAFIKIA HOTELI YAO ILE ILE TA KATIKATI YA YA JIJI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KIKOSI cha Yanga SC kimerejea Dar es Salaam jana jioni kutoka Morogoro, ambako kiliweka kambi tangu Jumanne kujiandaa na mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya mahasimu wa jadi, Simba kesho Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Yanga SC imeweka kambi katika hoteli ya Tiffany iliyopo katikati ya Jiji ambako kwa siku za karibuni ndipo wamekuwa wakiweka kambi zao kabla ya mechi zote muhimu.
    Kuna utulivu wa hali ya juu kwenye kambi ya Yanga na wachezaji wanaonekana kabisa kutulia kuelekeza fikra zao kwenye mchezo wa kesho.
    Kocha mpya, Mkongo Mwinyi Zahera anatumia muda huu mchache uliobaki kuzoeana na Wasaidizi wake, Mzambia, Noel Mwandila na wazawa Nsajigwa Shadrack na Juma Pondamali pamoja na wachezaji.
    Yanga SC wanateremka uwanja wa Taifa kesho mjini Dar es Salaam kumenyana na Simba katika mechi ya Ligi Kuu, ambayo wanahitaji ushindi ili kuweka hai matumaini ya ubingwa.
    Simba SC iliyo chini ya kocha Mfaransa, Pierre Lechantre anayesaidiwa na Mtunisia, Aymen Mohamed Hbibi, Mrundi, Masoud Juma na mzawa Muharami Mohamed ‘Shilton’ inaongoza Ligi Kuu kwa pointi zake 59 baada ya kucheza mechi 25, wakati Yanga inafuatia kwa mbali kidogo ikiwa na pointi zake 48 za mechi 23.
    Yanga inazidiwa pointi 11 na Simba SC na ina viporo viwili, maana yake ili kutetea ubingwa wao, itabidi washinde Jumapili na washinde mechi zao zote zilizobaki za Ligi Kuu, huku wakiwaombea mahasimu wao hao wapoteze mechi nyingine pia moja – jambo ambalo hakika ni gumu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC WAREJEA DAR KIMYA KIMYA, WAFIKIA HOTELI YAO ILE ILE TA KATIKATI YA YA JIJI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top