• HABARI MPYA

    Monday, April 30, 2018

    HANS POPPE AUNGANISHWA KESI YA AVEVA NA KABURU, MAHAKAMA YAMTAFUTA TANGU MACHI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam imewaongeza Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Pope na mkandarasi wa uwanja wa klabu hiyo, Frank Peter Lauwo katika kesi ya utakatishaji fesha na kugushi inayowakabili Rais wa klabu hiyo, Evans Aveva na makamu wake, Geofrey Nyange 'Kaburu'.
    Mahakama hiyo, imeagiza Hans Pope na Lauwo wakamatwe na kufikishwa mahakamani kujibu mashitaka yanayowakabili.
    Amri hiyo imetolewa na Hakimu Mkazi Mkuu Thomas Simba wa mahakama hiyo baada ya Swai kudai amewatafuta washitakiwa hao wamekuwa wakitafutwa tangu Machi mwaka huu bila mafanikio na kuomba hati ya kuwakamata.
    Kufuatia mabadiliko hayo washtakiwa,  wamesomewa upya hati ya mashtaka na wanakabiliwa na jumla ya mashtaka 10 tofauti na hati ya mashitaka ya awali iliyokuwa na mashtaka matano.
    Zacharia Hans Poppe (kulia) Mahakama inamtafuta tangu mwezi Machi

    Wakili wa Serikali kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Leornad Swai amedai kwamba, kesi hiyo leo ilikuja kwa ajili ya kuwasomea washitakiwa hao maelezo ya awali, lakini ameomba kufanywa mabadiliko ya hati ya mashitaka.
    Katika mashitaka hayo, washitakiwa wanakabiliwa na shitaka la kula njama, kutoa nyaraka za uongo, matumizi mabaya ya madaraka, kughushi, utakatishaji, kuwasilisha nyaraka za kughushi na kuendesha biashara bila kufuata sheria.
    Akisoma mashitaka hayo, Swai amedai kwamba, katika shitaka la kwanza, Aveva na Nyange, walikula njama ya kutenda kosa la kutumia madaraka vibaya na kati ya Machi 10 na 16 jijini Dar es Salaam, walitumia madaraka yao vibaya.
    Machi 15 mwaka 2016 wanadaiwa kuandaa fomu ya maombi ya kuhamisha dola za Kimarekani 300,000, karibu Sh. Milioni 700 kutoka kwenye akaunti ya Simba iliyopo CRDB tawi la Azikiwe kwenda kwenye akaunti binafsi ya Barclays kwa madhumuni ya kujipatia faida.
    Aidha, wote kwa pamoja waliwasilisha nyaraka ya kughushi, inadaiwa kuwa Aveva Machi 15, 2016 katika banki ya CRDB aliwasilisha nyaraka ya uongo ikionyesha Simba wanalipa mkopo wa dola za Kimarekani 300,000, takriban Sh. Milioni 700.
    Katika shitaka la utakatishaji fedha linalomkabili Aveva, imedaiwa Machi 15, 2016 katika benki ya Baclays Mikocheni, Dar es Salaam alijipatia dola za Kimarekani 187,817, takriban Sh. Milioni 400 kutoka wakati akijua zimetokana na zao la kosa la kughushi.
    Katika shitaka la sita, imedaiwa Nyange alimsaidia Aveva kujipapatia dola za Kimarekani 187,817, takriban Sh. Milioni 400 kutoka kwenye akaunti ya Simba wakiwa wanajua fedha hizo zimetokana na zao la kughushi
    Katika shitaka la saba la kughushi, linaloqakabili mstakiwa wa Aveva, Nyange na Poppe imedaiwa katika tarehe hizo hizo kwa pomoja walighushi hati ya malipo ya kibiashara ya Mei 28/ 2016 wakionyesha kwamba nyasi bandia zilizonunuliwa na Simba zinathamani ya dola 40,577, zaidi ya Sh. Milioni 90huku wakijua kwamba sio kweli.
    Katika shitaka la nane imedaiwa Aveva aliwasilisha hati ya madai (commercial invoice),  ya uongo kwa Levison Kasulwa ya Mei 28/ 2016 kwa madhumuni ya kuonyesha kwamba Simba wamenunua nyasi bandia zenye thamani ya USD 40,577
    Katika shitaka la tisa, Aveva, Nyange na Hans Poppe kati ya Machi 10 na Septemba 30, mwaka 2016 waliwasilisha nyaraka za uongo kuonyesha Simba imenunua nyasi bandia zenye thamani ya dola za Kimarekani 40,577.
    Katika shtaka la mwisho imedaiwa, kati ya Machi na Septemba 2016 Lauwo aliendesha biashara kama mkandarasi kwa kujenga uwanja wa Simba uliopo Bunju wakati akiwa hajasajiliwa
    Hata hivyo washtakiwa wamekana mashtaka hayo yote na wamepelekwa rumande kwa sababu shtaka la utakatishaji fedha linalowakabili halina dhamana.
    Kesi hiyo imahirishwa hadi Mei 14, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa na kufuatilia kama washitakiwa hao wawili watakuwa wamekamatwa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HANS POPPE AUNGANISHWA KESI YA AVEVA NA KABURU, MAHAKAMA YAMTAFUTA TANGU MACHI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top