• HABARI MPYA

    Friday, April 27, 2018

    NJOMBE MJI FC YAIPIGA NDANDA FC 2-0 NA KUJINASUA MKIANI, MBEYA CITY 1-1 SINGIDA UNITED

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Njombe Mji FC leo imetumia vizuri Uwanja wa nyumbani, Saba Saba mjini Njombe baada ya kuichapa mabao 2-0 Ndanda FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Ushindi huo uliotokana na mabao ya Notikeli Masasi na Ahmed Adwale unaifanya Njombe Mji FC ifikishe pointi 22 baada ya kucheza mechi 26 na kupanda kwa nafasi moja hadi ya 15 kutoka ya mwisho, sasa ikiwa mbele ya Maji Maji ya Songea yenye pointi 20 za mechi 25.
    Baada ya kichapo hicho, Ndanda FC inabaki nafasi ya 14 kwenye Ligi Kuu ya timu 16 ikiwa na pointi zake 23 za mechi 22, nyuma ya Mbao FC yenye pointi 24 za mechi 25.
    Nayo Mbeya City imelazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na Singida United Uwanja wa Sokine mjini Mbeya katika mchezo mwingine wa Ligi Kuu leo.
    Mbeya City ya kocha Mrundi, Ramadhani Nswazurimo ilitangulia kwa bao la beki wake wa kulia, Haruna Shamte dakika ya nne, kabla ya Singida ya kocha Mholanzi, Hans van der Pluijm kusawazisha kupitia kwa Malik Antiri dakika ya 17.
    Mbeya City inajiongezea pointi moja na kufikisha 28 baada ya kucheza mechi 26 ikiendelea kusimama nafasi ya tisa, wakati Singida United inafikisha pointi 39 baada ya kucheza mechi 26.
    Ligi Kuu itaendelea kesho kwa mechi tatu, Azam FC wakiwa wageni wa Mtibwa Sugar Uwanja wa Manungu, Turiani mjini Morogoro, Majimaji FC wakiwakaribisha Ruvu Shooting FC Uwanja wa Maji Maji mjini Songe na Stand United FC wakiwa wenyeji wa Kagera Sugar FC Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NJOMBE MJI FC YAIPIGA NDANDA FC 2-0 NA KUJINASUA MKIANI, MBEYA CITY 1-1 SINGIDA UNITED Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top