• HABARI MPYA

    Wednesday, April 04, 2018

    BEKI CHIPUKIZI DICKSON JOB ASAINI MKATABA MPYA WA MIAKA MITATU MTIBWA SUGAR

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    BEKI chipukizi wa Mtibwa Sugar, Dickson Job jana amesaini mkataba mpya wa miaka mitatu kuendelea kuichezea timu hiyo ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Katibu Msaidizi wa Mtibwa Sugar, Abubakar Swabur ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online kwamba Job ambaye alisimamiwa na kaka yake, George Job kwa sababu yeye mwenyewe hajafikisha umri wa miaka 18.
    “Kwa kweli mimi nimefurahi sana kupewa mkataba huu katika timu hii ambayo kihistoria imeibua nyota wengi wanaofanya vizuri hapa nchini na ninaahidi kuendelea kujituma ili nifanye vizuri na kuisaidia timu yangu,”alisema Job.

    Dickson Job amesaini mkataba mpya wa miaka mitatu kuendelea kuichezea Mtibwa Sugar
    Dickson Job (katikati) akisaini mkataba mpya Mtibwa Sugar. Kushoto ni Mkurugenzi wa Mtibwa, Jamal Bayser na kulia ni kaka yake, George Job
    Kutoka kushoto Dickson Job, Abubakar Swabur na George Job 

    Kwa upande wake, Swabur alisema kwamba Mtibwa Sugar inaendeleza sera zake za kuibua na kukuza vipaji vya wanasoka chipukizi nchini kwa kumpa mkataba mzuri Job.
    “Huu ndiyo umekuwa utamaduni wa Mtibwa kwa miaka mingi, kuchukua wachezaji wakiwa vijana wadogo na kuja kuuwalea huku. Nasi tunaahidi kuuendeleza, hatutaishia hapa lwa Job tu, hivi karibuni mtasikia zaidi,”alisema Swabur.  
    Job alikuwemo kwenye kikosi cha timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys kilichoshiriki fainali za Afrika (AFCON U17) nchini Gabon Mei mwaka jana na kwa sasa amepandishwa kwenye kikosi cha U20, Ngorongoro kinachoshiriki mechi za kufuzu AFCON U20 mwakani nchini Niger. 
    Lakini Ngorongoro Heroes imejiweka pagumu katika kinyang’anyiro cha tiketi ya Fainali za AFCON U20 mwakani Niger baada ya sare ya 0-0 na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Jumamosi kwenye mchezo wa kwanza wa Raundi ya Kwanza ya kufuzu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Kwa sare hiyo, Ngorongoro inayofundishwa na kocha Ammy Ninje anayesaidiwa na Juma Mgunda, Boniface Pawasa katika mazoezi ya nguvu, Meneja Leopold Mukebezi ‘Tassle’ na kicha wa makipa, Saleh Machuppa italazimika kwenda kushinda ugenini wiki mbili zijazo kwenye mchezo wa marudiano.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BEKI CHIPUKIZI DICKSON JOB ASAINI MKATABA MPYA WA MIAKA MITATU MTIBWA SUGAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top