• HABARI MPYA

    Monday, January 22, 2018

    SIMBA YAENDELEZA WIMBI LA USHINDI LIGI KUU, YAIBABUA KAGERA SUGAR 2-0 KAITABA

    Na Mwandishi Wetu, BUKOBA
    SIMBA SC imewapa raha mashabiki wake baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Kagera Sugar leo kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Kaitaba, Bukoba.
    Ushindi huo unaifanya Simba SC irejee kileleni mwa Ligi Kuu kwa kufikisha pointi 32 baada ya kucheza mechi 14, ikifuatiwa na Azam FC pointi 30 na mabingwa watetezi, Yanga SC pointi 25.
    Pongezi kwa wafungaji wa mabao ya Simba leo, wazawa kiungo Said Hamisi Ndemla na mshambuliaji na Nahodha John Raphael Bocco wote kipindi cha pili.
    Baada ya dakika 45 ngumu za kipindi cha kwanza, Ndemla aliwainua vitini mashabiki wa Simba SC dakika ya 69 kwa kufunga bao la kwanza akimalizia pasi ya kiungo wa pembeni, Shiza Kichuya.
    Wafungaji wa mabao ya Simba leo, Said Ndemla na John Bocco wakipongezana baada ya bao la kwanza 

    Mpira uliozaa bao hilo ulitokana na makosa ya mshambuliaji wa Kagera Sugar, Atuepe Green aliyepiga bila uangalifu ukanaswa na Bocco aliyekimbia nao pembezoni mwa Uwanja kulia kabla ya kutia krosi iliyumkuta mshambuliaji Mganda Emmanuel Okiw aliyempasia kwa kichwa Kichuya ambaye naye alimpa Ndemla aliyefunga. 
    Baada ya hapo, Kagera Sugar waliokuwa wakicheza kwa kujihami kwa muda mrefu na kushambulia kwa kuvizia, wakaamua kufunguka moja kwa moja kusaka bao la kusawazisha.
    Lakini hiyo nayo iliwagharimu kufungwa bao la pili kwa shambulizi la kujibiwa, beki Shomary Kapombe akimlamba chenga beki wa Kagera Sugar, Adeyoum Ahmed na kutia krosi nzuri iliyomaliziwa na Bocco kuipatia Simba bao la pili.
    Bocco aliye katika msimu wake wa kwanza Simba tangu asajiliwe kutoka Azam FC, aliweka rekodi ya kumfunga bao la 10 kipa mkongwe na hodari nchini, Juma Kaseja. Hiyo ni kuanzia Bocco akiwa Azam FC na Kaseja akichezea, Simba, Yanga na Mbeya City kabla ya kutua Kagera Sugar msimu uliopita.
    Kinara wa mabao wa Ligi Kuu, Emmanuel Okwi alikaribia kufunga bao la tatu dakika ya 90, lakini mpira ukaenda nje kidogo.  
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, Maji Maji ya Songea imelazimishwa sare ya 1-1 na Singida United Uwanja wa Maji Maji mjini Songea.
    Kikosi cha Kagera Sugar kilikuwa; Juma Kaseja, Eladius Mfulebe, Adeyum Ahmed, Juma Nyoso, Mohammed Fakhi, George Kavila, Pastory Athanas/Christopher Edward dk62, Ally Nassor ‘Ufudu’, Jafary Kibaya, Ally Ramadhan na Atupele Green/Peter Mwalyanzi dk80.
    Simba SC; Aishi Manula, Nicholas Gyan/Shomary Kapombe dk70, Asante Kwasi, Juuko Murshid, Erasto Nyoni, Jonas Mkude, James Kotei/Laudit Mavugo dk80, Shiza Kichuya/Muzamil Yassin dk90, Emmanuel Okwi, John Bocco na Said Ndemla.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA YAENDELEZA WIMBI LA USHINDI LIGI KUU, YAIBABUA KAGERA SUGAR 2-0 KAITABA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top