• HABARI MPYA

    Tuesday, January 23, 2018

    KOCHA WA MWADUI AANGUKA BAFUNI NA KUFARIKI DUNIA SHINYANGA LEO

    Na Mwandishi Wetu, MWADUI
    KOCHA Msaidizi wa Mwadui FC, Jumanne Ntambi (pichani kulia) amefariki dunia usiku wa leo baada ya kuanguka bafuni wakati anaoga nyumbani kwake Mwadui mkoani Shinyanga.
    Taarifa za awali zinasema mwalimu Ntambi baada ya kuanguka bafuni alikimbizwa hospitali ambako walikofika, wakasema tayari amekwishafariki dunia.
    Imeelezwa Ntambi alikuwa anasumbuliwa na shinikizo la damu na jana alikwenda hospitali kwa matibabu akaambiwa apumzike, ingawa leo aliwatembelea wachezaji mazoezini Uwanja wa Mwadui Complex.
    Mmoja wa wachezaji wa Mwadui FC, Athumani Maulid ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online usiku huu kwamba; “Tumepata msiba, kocha wetu Ntambi amefariki dunia usiku huu”.
    Maulid mmoja wa wachezaji wa timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys ya mwaka jana ameongeza; “Kocha alikuwa anaumwa na leo hakuja mazoezini kikazi. Alikuja tumekwishamaliza akatusalimia, tukazungumza naye, akaondoka ndipo baadaye zikaja taarifa za kifo chake,”amesema.
    Bado linasubiriwa tamko la Mwadui FC kuhusu utaratibu mzima wa mazishi ya marehemu, ambaye pamoja na kwamba familia yake ipo Moshi mkoani Kilimanjaro, yeye ni mzaliwa wa Musoma mkoani Mara.  Mungu ampumzishe kwa amani marehemu Jumanne Ntambi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KOCHA WA MWADUI AANGUKA BAFUNI NA KUFARIKI DUNIA SHINYANGA LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top