VIGOGO, Simba SC wameibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya wenyeji, Namungo FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Majaliwa, Ruangwa mkoani Lindi.
Mabao ya Simba SC yamefungwa na winga wa kushoto Msenegal, Libasse Guèye dakika ya 12, winga wa kushoto Muivory Coast, Alain Anicet Oura dakika ya 25 na winga wa kulia Mkongo, Elie Mpanzu Kibisawala dakika ya 74.
Bao pekee la Namungo limefungwa na mshambuliaji wa zamani wa Yanga SC, Heritier Ma Olongi Makambo dakika ya 33 kwa penalti.
Kwa ushindi huo, Simba SC inafikisha pointi 42, ingawa inabaki nafasi ya pili ilizidiwa pointi tano na mabingwa watetezi, Yanga SC baada ya timu zote kucheza mechi 19, wakati Namungo FC inabaki na pointi zake 22 za mechi 19 pia nafasi ya 10 kwenye ligi ya timu 16.
Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.
Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao.



.png)
0 comments:
Post a Comment