• HABARI MPYA

    Sunday, January 28, 2018

    DURU LA KWANZA LIGI KUU YA VODACOM TANZANIA BARA LAHITIMISHWA LEO

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    RAUNDI ya kwanza ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inahitimishwa leo kwa michezo miwili, vinara Simba SC wakiwakaribisha Maji Maji ya Songea Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam na Singida United watakuwa wenyeji wa Tanzania Prisons Uwanja wa Namfua mkoani Singida. 
    Kwa Simba SC mchezo wake wa leo una taswira mbili, kwanza ni kuendeleza wimbi la ushindi katika Ligi Kuu ili kumaliza kileleni baada ya duru la kwanza katika harakati zake za kutwaa ubingwa wa kwanza wa Ligi Kuu baada ya miaka mitano.
    Lakini pia ni kuwapa fursa mashabiki wake kujionea soka ya timu hiyo chini ya kocha mpya, Mfaransa Pierre Lechantre anayesaidiwa na Mrundi Masoud Juma, kocha wa viungo Mohamed Aymen Hbibi na kocha wa makipa  mzawa, Muharami Mohammed ‘Shilton’.

    Singida United wanaikaribisha Tanzania Prisons leo Uwanja wa Namfua mkoani Singida

    Lechantre alianza kazi Jumatano wiki hii Uwanja wa Chuo cha Bandari, Tandika mjini Dar es Salaam baada ya timu kurejea kutoka Bukoba ambako Jumapili iliyopita walishinda 2-0 dhidi ya wenyeji, Kagera Sugar chini ya kocha Masoud Juma.
    Na baada ya takriban siku tatu za kuweka ujuzi wake katika timu, mashabiki wa Simba wanatarajia kujionea mabadiliko fulani katika timu yao leo, ikicheza na timu dhaifu, Maji Maji. 
    Simba SC inaongoza Ligi Kuu kwa pointi zake 32, ikifuatiwa na Azam FC pointi 30 na Yanga SC pointi 28 ambazo zenyewe zimekamilisha mechi zake za duru la kwanza jana.
    Azam FC jana ilishindwa kutumia vyema Uwanja wa nyumbani baada ya kuchapwa mabao 2-1 na Yanga SC Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Israel Mujuni Nkongo aliyeyesaidiwa na washika vibendera Josephat Bulali na Soud Lila, ilibidi Yanga watoke nyuma baada ya mshambuliaji chipukizi, Shaaban Iddi Chilunda kutangulia kuifungia Azam FC bao la kuongoza dakika ya nne tu akimalizia krosi ya Mzimbabwe, Bruce Kangwa aliyemtoka beki Hassan Kessy pembeni na kuingia ndani.
    Yanga ilisawazisha kupitiaa kwa Mzambia Obrey Chirwa dakika ya 30 baada ya kupokea pasi ya kiungo mshambuliaji, Ibrahim Ajib na kumpiga chenga kipa wa Azam, Mghana Razack Abalora aliyetoka bila maarifa ya ziada, kabla ya beki Gardiel Michael Mbaga kufunga la ushindi dakika ya 44.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DURU LA KWANZA LIGI KUU YA VODACOM TANZANIA BARA LAHITIMISHWA LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top