• HABARI MPYA

    Friday, January 19, 2018

    MATELEMA APIGA HAT TRICK JKT TANZANIA YAREJEA LIGI KUU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya JKT Tanzania imejihakikishia kurejea Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu ujao baada ya ushindi wa mabao 5-1 dhidi ya African Lyon, zote za Dar es Salaam Uwanja wa Meja Jenerali Michael Isamuhyo, Mbweni JKT.
    Ushindi huo unaifanya JKT Tanzania ifikishe pointi 31 baada ya kucheza mechi 12 na kuendelea kuongoza Kundi A, ikifuatiwa kwa mbali na Friends Rangers yenye pointi 22 za mechi 12 pia kuelekea raundi mbili za mwisho.
    Katika mchezo huo, mabao ya JKT Tanzania yamefungwa na Salim Aziz Gilla dakika ya sita, Hasssan Matelema matatu dakika za 53, 64 na 80 na Ally Bilal dakika ya 78.
    Nyota wa JKT Tanzania, Hasssan Matelema (kushoto) akikabidhiwa mpira leo baada ya kufunga hat trick

    JKT Tanzania inafanikiwa kurudi Ligi Kuu baada ya msimu mmoja tu tangu iteremke na baada ya mchezo huo, Mwenyekiti wa timu, Luteni Kanali Hassan Mabena aliwapongeza Kocha Mkuu Bakari Shime na benchi lake zima la ufundi na wachezaji kwa kazi nzuri waliyoifanya.
    Baada ya JKT Tanzania, zamani JKT Ruvu kujihakikishia kurudi Ligi Kuu sasa inaziachia vita Friends Rangers yenye pointi 22 na Lyon yenye pointi  21 baada ya zote kucheza mechi 12 kupambana katika mechi mbili za mwisho kuwania nafasi moja iliyobaki katika kundi hilo kupanda.  
    Ligi Daraja la Kwanza Tanzania imegawanywa katika makundi matatu na kila kundi litatoa timu mbili za kupanda Ligi Kuu ambayo itateremsha timu mbili ili kuwa na timu 20 msimu ujao.
    Kundi B Coastal Union inaongoza kwa pointi zake 21, ikifuatiwa na JKT Mlale pointi 21 na Polisi Tanzania pointi 20, wakati Kundi C Biashara Mara inaongoza kwa pointi zake 23, ikifuatiwa na Dodoma FC pointi 21 na Alliance Schools pointi 19 baada ya timu zote kucheza mechi 11.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MATELEMA APIGA HAT TRICK JKT TANZANIA YAREJEA LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top