• HABARI MPYA

    Sunday, October 22, 2017

    SAMATTA AFIKISHA MECHI TISA BILA KUFUNGA GENK YASHINDA 1-0 UGENINI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta leo amecheza mechi ya tisa bila kufunga bao katika klabu yake, KRC Genk ingawa imeibuka na ushindi wa 1-0 ugenini dhidi ya Anderlecht kwenye mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji Uwanja wa Constant Vanden Stock mjini Brusells.
    Bao pekee la ushindi la Genk limefungwa na beki kinda wa umri wa miaka 22, Mghana Joseph Aidoo dakika ya 50 akimalizia kazi nzuri ya mshambuliaji Mbelgiji, Siebe Schrijvers.
    Mbwana Samatta (kulia) amecheza dakika zote 90 leo KRC Genk ikishinda 1-0 ugenini dhidi ya Anderlecht  

    Samatta leo amecheza mechi ya 67 katika mashindano yote tangu Januari mwaka jana alipojiunga na Genk akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Katika mechi hizo, Samatta ambaye ni mshindi wa tuzo ya Mwanasoka Bora Anayecheza Afrika mwaka jana alipokuwa na Mazembe, 39 ameanza na mechi 24 ametokea benchi, akifunga jumla ya mabao 21 kwenye mashindano yote.
    Mara ya mwisho Samatta alifunga mabao mawili Genk Agosti 13, mwaka huu ikishinda 5-3 dhidi ya wenyeji, Royal Antwerp FC katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji Uwanja wa Bosuilstadion, Deurne.
    Kikosi cha RSC Anderlecht kilikuwa; Boeckx, Kara, Dendoncker, Deschacht, Appiah/Harbaoui dk69, Onyekuru, Trebel, Kums, Gerkens/Bruno dk77, Hanni/Obradovic dk69 na Teodorczyk.
    KRC Genk : Vukovic, Uronen, Colley, Aidoo, Mata, Berge, Malinovskyi/Khammas dk92, Pozuelo/Buffalo dk87, Writers, Samatta na Ingvartsen/Heynen dk84.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA AFIKISHA MECHI TISA BILA KUFUNGA GENK YASHINDA 1-0 UGENINI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top