• HABARI MPYA

    Monday, October 23, 2017

    YANGA YABAKI SHINYANGA, KUONDOKA KWA BASI KESHO KUREJEA DAR

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KIKOSI cha Yanga kimebaki Shinyanga kwa mapumziko ya siku moja baada ya ushindi wa jana wa 4-0 dhidi ya wenyeji, Stand United kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Msemaji wa Yanga, Dissmas Ten ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online leo kwamba timu itaondoka Shinyanga kesho kwa basi kurejea Dar es Salaam na inaweza kuingia kambini kuanzia Jumatano kujiandaa na mchezo ujao dhidi ya Simba.
    Yanga watamenyana na mahasimu wao wa jadi, Simba katika mchezo mwingine wa Ligi Kuu Jumamosi Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam, ambao unasubiriwa kwa hamu na mashabiki wa soka nchini. 
    Na ilitarajiwa Yanga ingendoka mara tu baada ya mchezo wa jana kwenda Mwanza kuunganisha ndege kuwahi Dar es Salaam kwa mipango ya kambi ya mechi dhidi Simba Oktoba 28.
    Tofauti na matarajio hayo, Ten amesema kikosi kitafanya mazoezi leo Shinyanga na kesho mapema ndio kitaondoka mkoani humo kurejea Dar es Salaam – maana yake timu itafika kesho usiku kama hawatapata matatizo yoyote njiani na mipango yoyote ya kambi inaweza kuanza Jumatano.
    Kwa ratiba hii, uwezekano wa Yanga kwenda kwenye kambi yake maarufu ya Pemba kwa maandalizi ya mchezo huu ni mdogo, kwa sababu kutoka Jumatano hadi Jumamosi ni siku mbili tu kabla ya mchezo dhidi ya Simba.
    Mahasimu wao, Simba nao baada ya ushindi wa 4-0 dhidi ya Njombe Mji Jumamosi Uwanja wa Uhuru, mapema leo wameondoka kwenda Zanzibar kuweka kambi.
    Ikumbukwe Yanga iliondoka Dar es Salaam kwa ndege kwenda Bukoba kwa michezo yake miwili ya Kanda ya Ziwa, ikianza kwa ushindi wa 2-1 dhidi ya Kagera Sugar Uwanja wa Kaitaba kabla ya kupitiliza hadi Tabora ambako iliweka kambi ya kujiandaa na mchezo dhidi ya Stand pamoja na kucheza mechi ya kirafiki pia na wenyeji, Rhino Rangers wakitoa sare ya 0-0.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA YABAKI SHINYANGA, KUONDOKA KWA BASI KESHO KUREJEA DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top