Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
RASMI klabu ya Yanga imetangaza kumsajili kipa Mcameroon, Youthe Rostand ambaye msimu uliopita aliidakia African Lyon katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
Pamoja na Lyon kuteremka daraja baada ya msimu, lakini bado Yanga ilivutiwa na udakaji wa mlinda mlango huyo na kuamua kumrudisha Ligi Kuu.
Hii si mara ya kwanza Yanga kusajili kipa wakati timu yake imetoka kushuka daraja, kwani mwaka 1993 ilimsajili Steven Nemes baada ya klabu yake, Nyota Nyekundu, iliyokuwa ikijulikana pia kama Red Star kushuka Daraja msimu wa 1992.
Youthe Rostand (kushoto) akisaini mkataba wa kujiunga na Yanga SC kutoka African, zote za Dar es Salaam
Mwaka 2010 ikamsajili kipa Said Mohammed Mduda akitoka Maji Maji ya Songea iliyoshuka Daraja pia na sasa inarudia tena, ingawa safari hii ni kwa kipa mgeni.
Rostand anakuwa mchezaji wa nne kusajiliwa rasmi Yanga katika dirisha hili kubwa, baada ya beki Abdallah Hajji ‘Ninja’ kutoka Taifa Jang’ombe, kiungo Pius Buswita kutoka Mbao FC na mshambuliaji Ibrahim Hajib kutoka Simba.
0 comments:
Post a Comment