• HABARI MPYA

    Saturday, June 03, 2017

    HOMA YA SPORTPESA SUPERCUP, SIMBA YAINGIA KAMBINI

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Simba SC imerudi kambini leo kwa ajili ya kujiandaa na mashindano ya SportPesa Super Cup yanayotarajiwa kuanza Juni 5, mwaka huu kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online leo, Mratibu wa Simba SC, Abbas Ally amesema kwamba timu hiyo imeingia kambini leo katika hoteli ya Sapphier Court mjini Dar es Salaam.
    "Timu imeingia kambini leo na tumefanya mazoezi leo asubuhi na wachezaji wote ambao hawajaitwa kwenye timu ya taifa wamekwishawasili kambini,"amesema Ally.  
    Mratibu huyo amesema kwamba wanayapa uzito mashindano hayo kama mashindano yote waliyowahi kushiriki na lengo lao ni kubeba Kombe.  
    “Mashindano haya ni makubwa, ukiangalia zimeshirikishwa nchi tofauti kwa hivyo ni mashindano makubwa na sisi kama Simba tunayaheshimu mashindano haya,”amesema.
    Akizungumzia uchache wa wachezaji kwa kuwa wachezaji wengine wameitwa kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars amesema kwamba, ni fursa nzuri kwa wachezaji waliobaki kuuonyesha uwezo wao ili kumshawishi kocha aendelee kuwa nao kikosini.
    Bingwa wa michuano hiyo atapata dola za Kimarekani 30,000, zaidi ya Sh. Milioni 60 za Tanzania na nafasi ya kucheza dhidi ya Everton ya England.
    Timu zinazoshiriki michuano hiyo ni Simba SC, Yanga SC na Singida United kwa Tanzania Bara, Jang'ombe Boys ya Zanzibar, Gor Mahia, AFC Leopards, Nakuru All Stars na Tusker FC za Kenya na mechi zote zitachezwa Uwanja wa Uhuru, Dar ea Salaam kuanzia Juni 5 hadi 11, mwaka huu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HOMA YA SPORTPESA SUPERCUP, SIMBA YAINGIA KAMBINI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top