• HABARI MPYA

    Wednesday, June 28, 2017

    NGOMA ABAKI YANGA, ASAINI MIAKA MIWILI LEO

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Zimbabwe, Donald Dombo Ngoma amesaini mkataba mpya wa miaka miwili kuendelea kuichezea Yanga SC.
    Ngoma aliwasili jana usiku Dar es Salaam baada ya taarifa kwamba amesaini mkataba wa miaka mitatu kujiunga na Polokwane City ya Afrika Kusini.
    Lakini tangu jana mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 27 amekuwa kwenye mazungumzo na uongozi wa Yanga kabla ya leo mchana kusaini, hivyo pia kuzima tetesi za kwamba anataka kujiunga na mahasimu, Simba. 
    Mshambuliaji Mzimbabwe, Donald Dombo Ngoma aksaini mkataba wa miaka miwili leo mjini Dar es Salaam kuendelea kuichezea Yanga na kuzima tetesi za kwenda Polokwane City au Simba
    Katika miaka yake miwili ya kwanza, Ngoma alikuwa ana msimu wa kwanza mzuri Yanga SC, akiiongoza kutwaa mataji yote matatu, Ngao ya Jamii, Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), au Azam Sports Federation Cup (ASFC) na kuiwezesha pia kufuzu hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika, baada ua kutolewa 16 Bora Ligi ya Mabingwa.
    Hata hivyo, msimu wake wa pili Ngoma hakuwa mzuri Yanga kutokana na kusakamwa na maumivu ya goti, huku timu yake ikiweza tu kutetea taji Ligi Kuu na kuvuliwa mengine ya Ngao ya Jamii iliyochukuliwa na Azam na ASFC lililobebwa na Simba.
    Na hata katika michuano ya Afrika, Yanga haikuweza kurudia mafanikio yake ya msimu uliopita baada ya kushindwa kufuzu hatua ya makundi.
    Ngoma aliyezaliwa Kwekwe, Zimbabwe alijiunga na Yanga SC mwaka 2015 akitokea FC Platinum ya kwao, aliyoanza kuichezea mwaka 2012 akitokea Monomotapa United iliyomuibua mwaka 2011.
    Amewahi kuitwa timu ya taifa ya Zimbabwe mara kadhaa tangu mwaka 2011na hadi sasa amecheza mechi nane na kufunga mabao matatu. Na kwa kusaini Yanga, maana yake ataendelea kufanya kazi na rafiki zake, kiungo Mzimbabwe Thabani Kamusoko na mshambuliaji Mzambia, Thabani Kamusoko.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NGOMA ABAKI YANGA, ASAINI MIAKA MIWILI LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top