• HABARI MPYA

    Tuesday, June 20, 2017

    ALLY YANGA AFARIKI AJALINI KWENYE MBIO ZA MWENGE

    Na Mwandishi Wetu, DODOMA
    MWANACHANA wa klabu ya Yanga na mpenzi maarufu wa soka nchini, Ally Mohamed anayejulikana zaidi kwa jina la utani ‘Ally Yanga’ amefariki dunia leo baada ya ajali ya gari iliyotokea, eneo la Mpwapwa, Dodoma.
    Taarifa zinasema Ally Yanga alikuwa kwenye msafara wa mbio za Mwenge kabla ya kupata ajali hiyo barabara ya Wiyenzele kuelekea Chipogoro na kufariki hapo hapo.
    Ally aliyezaliwa mkoani Shinyanga Machi 1, mwaka 1984 katika familia ya watoto sita, kabla ya umauti wake inafahamika alikuwa anaishi Yombo Vituka, Dar es Salaam.
    Picha ndogo kulia ni Ally Yanga enzi za uhai wake. Na picha kubwa ni gari ambayo imesababisha kifo chake

    Aliibukia Ubungo miaka ya nyuma kidogo ambako alikuwa anafanya shughuli ya kusajili laini za simu za mkononi katika vibanda vilivyokuwa pembeni ya kituo kikuu cha mabasi ya mikoani, Ubungo Terminal.
    Na alianza kuonekana Uwanja wa Taifa pamoja na kikundi cha mashabiki wa Yanga cha Ubungo Terminal, ambako ndipo lilipokuwa tawi lake.
    Ally Yanga enzi za uhai wake akiishabiki Yanga Uwanja wa Taifa katika mechi tofauti
    Lakini tangu baada ya uchaguzi Mkuu Novemba 2015, Ally Yanga ameadimika viwanja vya soka kutokana na kujikita zaidi kwenye shughuli za Chama cha Mapinduzi CCM.
    Ally hakuwa shabiki wa Yanga tu, enzi za uhai wake alikuwa akizishabiki pia timu za taifa, kuanzia za vijana na wakubwa za wanawake na wanaume. 
    Alikuwa maarufu Afrika Mashariki kutokana na kwenda kuishabikia Taifa Stars kwenye mechi za Kombe la CECAFA Callenge nchi za Kenya na Uganda. Lakini pia amewahi kusafiri hadi nje ya Afrika ya Afrika Mashariki akiwa na Taifa Stars kwenye mechi za kufuzu Fainali za Mataifa ya Afrika na Kombe ka Dunia. Mungu ampumzishe kwa amani Ally Yanga. Amin.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ALLY YANGA AFARIKI AJALINI KWENYE MBIO ZA MWENGE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top