• HABARI MPYA

    Wednesday, June 28, 2017

    AVEVA, KABURU NAO WANASHIKILIWA NA TAKUKURU, YADAIWA SABABU YA FEDHA ZA OKWI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    RAIS wa Simba SC, Evans Elieza Aveva na Makamu wake, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ wanashikiliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kwa uchunguzi juu ya tuhuma za kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kutokana na mchezaji Emmanuel Okwi.
    Taarifa kutoka Simba zinasema kwamba viongozi hao wakuu wa klabu wamechukuliwa leo kwa wakati tofauti kwa ajili ya mahojiano juu ya tuhuma hizo.
    Inadaiwa kulikuwa kuna udanganyifu katika mauzo ya mchezaji Emmanuel Okwi kwenda klabu ya Esperance ya Tunisia kwamba kiasi kilichotajwa dola za Kimarekani 300,000, zaidi ya Sh. Milioni 600 si ambacho Simba ilipata katika biashara hiyo.
    Rais wa Simba SC, Evans Elieza Aveva na Makamu wake, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ wanashikiliwa na TAKUKURU

    Taarifa zinasema Simba ilipata fedha zaidi kwenye biashara hiyo iliyochukua muda mrefu kukamilika, lakini katika kumbukumbu za klabu ikaandikishwa dola 300,000 tu.
    Na ni kutokana na tuhuma hizo, TAKUKURU sasa inawashikilia viongozi hao wakuu wa klabu. Lakini Aveva hakuwapo madarakani wakati Simba inamuuza Okwi mwaka 2013, bali Kaburu alikuwa Makamu wa Rais, chini ya Rais wa wakati huo, Alhaj Ismail Aden Rage.
    Hata hivyo, Esperance ilichelewa kulipa fedha hizo na hadi Machi mwaka jana, wakati huo tayari Aveva ni Rais wa klabu na Kaburu ni Makamu wake, baada ya Rage kutogombea tena.
    Okwi alinunuliwa na Etoile Januari mwaka 2013, miaka mitatu tu baada ya kujiunga na Simba mwaka 2010, lakini baada ya miezi mitatu akatofautiana na klabu ya Tunisia kufuatia na kufungua kesi FIFA akiomba aruhusiwe kucheza klabu nyingine kulinda kipaji chake wakati mgogoro wake na Etoile unaendelea.
    Etoile ilisitisha huduma kwa Okwi, baada ya kukerwa na desturi ya mchezaji huyo kuchelewa kurejea kujiunga na timu kila alipokuwa anaporuhusiwa kwenda kujiunga na timu yake ya taifa Uganda.
    Akasaini tena SC Villa katikati ya mwaka 2013 kabla ya Desemba mwaka huo, kuhamia Yanga SC- wakati wote huo kesi yake na Etoile ikiendelea FIFA na Simba walikuwa hawajalipwa fedha zao.
    Simba nayo ilifungua kesi FIFA ikisistiza kulipwa fedha zake baada ya kumuuza mchezaji huyo Etoile Januari 2013.
    Okwi na Simba wakaungana tena mwaka 2014 baada ya mchezaji huyo kutofautiana na Yanga pia, akidai ilishindwa kummalizia fedha zake za usajili, hivyo Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kumruhusu kuondoka, naye akarejea Msimbazi.
    Kabla haijapata fedha za kumuuza Okwi Etoile, Simba ikamuuza tena Okwi klabu ya Sonderjyske ya Denmark kwa dau la  dola za Kimarekani 110,000 zaidi ya Sh. Milioni 230 za Tanzania.
    Hata hivyo, Denmark nako aliposaini mkataba wa miaka mitano, aliondoka baada ya miaka miwili tu na kurejea SC Villa mapema mwaka huu, kabla ya juzi kusaini mkataba wa miaka miwili kujiunga tena na Siumba kwa mara ya tatu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AVEVA, KABURU NAO WANASHIKILIWA NA TAKUKURU, YADAIWA SABABU YA FEDHA ZA OKWI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top