• HABARI MPYA

    Saturday, April 08, 2017

    YANGA WAWAINGIA WAARABU NA 4-3-3, NGOMA NJE, CHIRWA ANAANZA NA MSUVA

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MZAMBIA Obrey Chirwa ndiye atakuwa mshambuliaji kiongozi wa Yanga katika mchezo wa kwanza wa mchujo wa kuwania kucheza hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika leo dhidi ya Mouloudia Club Alger ya Algeria Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.  
    Kocha Mzambia, George Lwandamina tayari ametoa orodha ya wachezaji 11 wanoanza leo pamoja na sita watakaoanzia benchi.  
    Kikosi kimerudi karibu kile kile kilichoshinda 1-0 dhidi ya Azam katika mchezo uliopita wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara isipokuwa tu anakosekana kiungo Mzambia, Justin Zulu ambaye ni majeruhi. 
    Na badala yake leo ameendelea kucheza kiungo chipukizi, Said Juma ‘Makapu’ aliyempokea Jumamosi ya wiki iliyopita baada ya kuumia.
    Obrey Chirwa anaanza leo kama mshambuliaji kiongozi Yanga

    Lwandamina ametumia mfumo wa 4-3-3 akiwapanga Simon Msuva, Obrey Chirwa na Deus Kaseke kushambulia, wakati katika nafasi ya kiungo wapo Mnyarwanda Haruna Niyonzima, Thabani Kamusoko na Said Juma.
    Langoni yupo kama kawaida ‘Yanga One’, Deogratius Munishi ‘Dida’, beki ya kulia Hassan Kessy, kushoto Mwinyi Hajji Mngwali na katikati Mtogo Vincent Bossou na Nahodha Nadir Haroub ‘Cannavaro’.
    Katika benchi wapo kipa Beno Kakolanya, mabeki Juma Abdul, Vincent Andrew ‘Dante’, viungo Emmanuel Martin, Geoffrey Mwashiuya na mshambuliaji Mzimbabwe Donald Ngoma.
    Mchezo huo unaotarajiwa kuanza Saa 10:00 jioni, utachezeshwa na marefa kutoka Rwanda, Louis Hakizimana atakayepuliza filimbi akisaidiwa na washika vibendera Theogene Ndagijimana na Jean Bosco Niyitegeka, wakati refa wa akiba atakuwa Ruzindana Nsoro na Kamisaa ni Ata Elmanan Hassan Osama kutoka Sudan. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA WAWAINGIA WAARABU NA 4-3-3, NGOMA NJE, CHIRWA ANAANZA NA MSUVA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top