• HABARI MPYA

    Tuesday, April 25, 2017

    SERENGETI BOYS YADHIHIRISHA UBABE KWA GABON

    Na Mwandishi Wetu, RABAT
    TIMU ya soka ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys leo imedhihirisha ubabe wake kwa wenyeji wa fainali za U-17 Afrika mwaka huu, Gabon baada ya kuwafunga tena 2-1 katika mchezo wa kirafiki mjini Rabat.
    Mabao ya Serengeti Boys leo yamefungwa na Assad Juma na Abdul Hussein na hicho kinakuwa kipigo cha pili mfululizo vijana wa Tanzania wanawapa wavulana w Gabon, baada ya Aprili 22 kuwafunga pia 2-1, mabao ya Kelvin Nashon Naftali dakika ya 18 na Ibrahim Abdallah Ally dakika ya 75.
    Serengeti Boys imeweka kambi ya mwezi mmoja nchini Morocco kujiandaa na Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa vijana chini ya umri wa miaka 17, zinazotarajiwa kuanza Mei 14 hadi 28, mwaka huu nchini Gabon.
    Kwa ujumla huo unakuwa mchezo wa tano wa maandalizi kwa Serengeti kujiandaa fainali za Gabon, baada ya awali kuifunga Burundi mara mbili, Machi 30 mabao 3-0 na Aprili 1 mabao 2-0, mechi zote mbili zikipigwa Uwanja wa Kaitaba, Bukoba, kabla ya kulazimishwa sare ya 2-2 na Ghana ‘Black Starlets’ Aprili 3 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Serengeti Boys itakuwa kambini mjini Rabat hadi Mei 1, mwaka huu itakapowenda Younde, Cameroon kucheza mechi mbili za kirafiki dhidi ya wenyeji Mei 3 na 6, mwaka huu.
    Mei 7 timu hiyo itakwenda Gabon ambako imepangwa kundi B pamoja na timu za Mali, Niger na Angola, wakati Kundi A lina timu za wenyeji, Gabon, Guinea, Cameroon na Ghana. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERENGETI BOYS YADHIHIRISHA UBABE KWA GABON Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top