• HABARI MPYA

    Monday, April 24, 2017

    YANGA WAZINDUA AKAUNTI YA WANACHAMA KUCHANGIA KLABU, TIMU KWENDA DODOMA KESHO KWA MCHEZO WA KIRAFIKI

    Na Steven Kinabo, DAR ES SALAAM
    YANGA SC leo imezindua utaratibu wa wanachama wake kuichangia klabu kupitia simu za mikononi ambao utasimamiwa na kampuni ya Selcom ya Dar es Salaam.
    Katibu Mkuu wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa amesema leo katika mkutano na Waandishi wa Habari mjini Dar es Salaam kwamba utaratibu huo unaanza mara moja.
    Mkwasa ambaye ni mchezaji na kocha wa zamani wa Yanga, aliitaja namba ya kuchangia kuwa ni 150334 ambayo watumiaji wa mitandao yote ya simu za mkononi wanaweza kuitumia kuchangia klabu yao.
    Mkwasa amesema kwamba wameingia mkataba wa awali wa majaribio na Selcom kwa miezi mitatu na watakapoona zoezi hilo lina manufaa kwao, wataongeza mkataba. 
    “Huu ni mkataba wa awali tu wa majaribio na tutakapoona zoezi hili linakwenda vizuri, baso tutakaaa chini na wenzetu kufikiria namna ya kuongeza,”alisema.
    Charles Boniface Mkwasa (kushoto) akizungumza na Waandishi wa Habari leo makao makuu ya klabu, Jangwani, Dar es Salaam. Kulia ni mwakilishi wa Selcom, Gallus Runyeta

    Kwa upande wake, mwakilishi wa Selcom, Gallus Runyeta alisema kwamba wana matumaini zoezi hilo litafanikiwa sana na Yanga watafutahia.
    “Sisi kama Selcom tunafurahi kuingia katika ndoa hii na Yanga ambayo ni klabu kongwe na wapenzi wengi hapa nchini, na tunawaomba watu wote wenye mapenzi na Yanga wajitokeze sasa na kuanza kuichangia klabu yao,”alisema Gallus. 
    Wakati huo huo: Mkwasa amesema kwamba kikosi cha Yanga kitaondoka kesho Dar es Salaam kwenda Dodoma kwa mchezo mmoja wa kirafiki kikiwa njiani kuelekea Mwanza, ambako Jumapili kitakuwa na mchezo wa mashindano.
    Yanga watamenyana na Kombaini ya Majeshi Uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma Jumatano, kabla ya Jumapili kuwa wageni wa Mbao FC Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza katika Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Kombe la Azam Sporrs Federation (ASFC).
    Na mapema Jumatatu kikosi hicho kinatarajiwa kuendelea Dar es Salaam kuendelea na maandalizi ya mechi zake za viporo za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA WAZINDUA AKAUNTI YA WANACHAMA KUCHANGIA KLABU, TIMU KWENDA DODOMA KESHO KWA MCHEZO WA KIRAFIKI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top