• HABARI MPYA

    Friday, April 28, 2017

    JOHN BOCCO NI MTU HATARI INAPOKUJA AZAM NA SIMBA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SIKU mbili zijazo, Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, itakuwa kwenye kibarua kizito kusaka fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup) itakapokabiliana na Simba, katika mchezo wa nusu fainali ya michuano hiyo utakofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam Jumamosi ijayo.
    Azam FC ambayo inaendelea na maandalizi makali kuelekea mchezo huo ili kuhakikisha inatinga fainali kwa kuichapa Simba, itashuka dimbani katika mechi yake ya 26 ya mashindano yote dhidi ya Wekundu hao.
    Lakini hii itakuwa ni mara ya kwanza kihistoria kwa timu hizo kukutana katika michuano hiyo, ambayo ilirejeshwa msimu uliopita kufuatia kukosekana kwa misimu kadhaa.
    John Bocco akikimbilia mpira dhidiya beki wa Simba, Method Mwanjali kwenye mchezo wa Ligi Kuu baina ya timu hizo

    Kikosi cha Azam FC kipo kwenye hali nzuri kuelekea mchezo huo, na itanufaika na urejeo wa wachezaji wake kadhaa ambao waliokuwa majeruhi jambo ambalo limeongeza morali kikosini na kila mchezaji akiwa na hamu ya kufanya vema kwenye mtanange huo ili kuibeba timu hiyo na kusonga mbele.
    Wachezaji wanaorejea ni nahodha John Bocco ‘Adebayor’, mabeki Aggrey Morris, Yakubu Mohammed na kiungo Stephan Kingue, ambao kwa sasa wanaendelea na mazoezi na wenzao na limebakia suala la benchi la ufundi kuthibitisha kwamba wako tayari kwa mapambano au la.
    Itakumbukwa kuwa hiyo ndio nafasi pekee iliyobakia kwa mabingwa hao wa Ngao ya Jamii na Kombe la Mapinduzi msimu huu ya kukata tiketi kushiriki michuano ya Afrika mwakani, ambapo ikiingia fainali itakuwa imetanguliza mguu mmoja kwenye kuwania nafasi ya kushiriki Kombe la Shirikisho Afrika mwakani.
    Hadi inaingia fainali, Azam FC ilizitoa Cosmopolitan (3-1), Mtibwa Sugar (1-0) na kwenye robo fainali iliichapa Ndanda mabao 3-1.
    Kuelekea mtanange huo, tunakuletea rekodi mbalimbali baina ya timu hizo zilipokutana katika mechi za mashindano mbalimbali huko nyuma.
    Rekodi zao
    Wakati msimu huu ukielekea ukingoni, tayari timu hizo zimekutana mara tatu na Azam FC ikiwa kifua mbele baada ya kushinda mechi mbili na kupoteza moja, mechi hizo mbili ilizoibuka kidedea ya kwanza ilishinda kwenye fainali ya Kombe la Mapinduzi (1-0) kabla ya kupata ushindi kama huo kwenye Ligi Kuu, huku Simba nayo ikishinda ya mzunguko wa kwanza 1-0.
    Hivyo wakati timu hizo zikielekea kucheza kwenye mechi yao ya nne msimu huu, kihistoria zimekutana mara 25 katika michuano mbalimbali huko nyuma, Azam FC ikishinda mara tisa, Simba mara 11 huku ikishuhudiwa mechi tano wakienda sare.
    Bocco hashikiki
    Bocco ndiye mchezaji pekee hapa nchini kihistoria, ambaye anashikilia rekodi kufunga mabao mengi kwenye mechi za watani wa jadi, kila anapokutana na Simba na Yanga, mpaka sasa akiwa amefunga jumla ya mabao 34.
    Katika mchanganuo wa mabao hayo, Bocco ameifunga Simba mabao 19 kwenye mechi mbalimbali walizokutana na Yanga akiitupia 15, rekodi ambayo inamfanya kuwa mchezaji wa kuogopwa kuelekea mtanange huo.
    Bocco ambaye ameshafunga bao moja katika michuano hiyo wakati Azam FC ikiichapa Cosmopolitan, tayari amefunga jumla ya mabao 10 kwenye mashindano mbalimbali, nane Ligi Kuu, moja FA Cup na jingine akitupia wakati matajiri hao wakitwaa Ngao ya Jamii mwanzoni mwa msimu kwa kuifunga Yanga kwa mikwaju ya penalti 4-1 kufuatia sare ya 2-2.
    Mshambuliaji kinda Shaaban Idd, ndiye kinara wa kufumania nyavu kwa upande wa Azam FC kwenye michuano hiyo, akiwa ametupia matatu, moja dhidi ya Cosmopolitan na mawili akitupia wakati wakiitoa Ndanda.
    Mwingine anayefuatia ni winga Ramadhan Singano ‘Messi’, ambaye ameshafunga mawili kwenye ushindi wa 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar na jingine dhidi ya Ndanda, huku Joseph Mahundi naye akiwa na bao moja, alilopachika dhidi ya Cosmopolitan.

    Dondoo za mechi zote
    1. LIGI KUU MARA 18
    -Simba wameshinda 8
    -Azam wameshinda 5
    -Sare mara 5
    2. NGAO YA JAMII MARA 1
    -Simba 3-2 Azam FC (2012)
    3. MAPINDUZI CUP MARA 3
    -Azam 2-0 Simba - 2011 nusu fainali
    -Azam 2-2 Simba (pen 5-4) - 2012 nusu fainali
    -Azam 1-0 Simba - (2017 fainali)
    4. KAGAME CUP MARA 1
    -Azam 3-1 Simba - 2012 robo fainali
    5. KOMBE LA UJIRANI MWEMA MARA 1
    -Simba 2-2 Azam(pen 4-3) - fainali 2012
    6. ABC SUPER 8 - MARA 1
    -Simba 2-1 Azam - nusu fainali 2012
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: JOHN BOCCO NI MTU HATARI INAPOKUJA AZAM NA SIMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top