• HABARI MPYA

    Saturday, April 22, 2017

    DIDA ACHOMOA, KAKOLANYA ANAANZA LEO YANGA NA PRISONS

    Na Steven Kinabo, DAR ES SALAAM
    MLINDA mlango wa tatu wa Yanga, Benno Kakolanya ndiye akayedaka leo dhidi ya timu yake ya zamani, Prisons katika Robo Fainali ya mwisho ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), au Azam Sports Federation Cup (ASFC) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Kipa wa kwanza, Deo Munishi ‘Dida’ aliyekuwa katika mipango ya kuanza leo, ameamka asubuhi na kusema hajisikii vizuri, hivyo kocha Mzambia George Lwandamina amelazimika kumuanzisha Kakolanya kwa kuwa kipa wa pili, Ally Mustafa 'Barthez' hayuko vizuri pia.  
    Deo Munishi 'Dida' hajisikii vizuri leo na ameomba apumzike, hivyo Benno Kakolanya ataanza 

    Mabeki Juma Abdul, Vincent Bossou, viungo Haruna Niyonzima, Deus Kaseke na mshambuliaji Donald Ngoma watakosekana katika mchezo wa leo kwa sababu mbalimbali, wengi wao wakisema wanaumwa, lakini inadhaniwa ni migomo ya kushinikiza walipwe malimbikizo ya mishahara yao.
    Kwa ujumla kikosi cha Yanga kitakachomenyana na Prisons kuanzia Saa 10:00 jioni ya leo kipo hivi; Benno Kakolanya, Hassan Kessy, Mwinyi Hajji Mngwali, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Said Juma ‘Makapu’, Simon Msuva, Thabani Kamusoko, Obrey Chirwa, Amissi Tambwe na Geoffrey Mwashiuya.
    Katika benchi watakuwapo ⁠⁠Dida, Oscar Joshua, Andrew Vincent ‘Dante’, Emmanuel Martin, Juma Mahadhi, Matheo Anthony na Yussuf Mhilu.
    Yanga wanaingia kwenye mchezo wa leo wakitoka kutolewa kwenye michuano ya klabu Afrika, baada ya kufungwa 4-0 na MC Alger Jumamosi iliyopita mjini Algiers hivyo kutupwa nje katika kinyang'anyiro cha tiketi ya makundi Kombe la Shirikisho kwa jumla ya mabao 4-1, baada ya kushinda 1-0 kwenye mchezo wa kwanza Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DIDA ACHOMOA, KAKOLANYA ANAANZA LEO YANGA NA PRISONS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top