• HABARI MPYA

    Wednesday, April 26, 2017

    MAKAMU WA RAIS TFF AHUDHURIA MAZOEZI YA SIMBA MOROGORO

    Na Mwandishi Wetu, MOROGORO
    MAKAMU wa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wallace Karia leo amehudhuria mazoezi ya klabu ya Simba mjini Morogoro.  
    Simba imeweka kambi Morogoro tangu juzi kujiandaa na mchezo wa Nusu Fainali ya Kombe la  TFF, maarufu kama Kombe la Azam Sports Federation (ASFC) dhidi ya Azam FC Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Na Karia leo alikuwa Uwanja wa Jamhuri Morogoro pamoja na viongozi wa Simba SC, wakiongozwa na Rais wa klabu hiyo, Evans Elieza Aveva kujionea maandalizi ya timu hiyo.
    Makamu wa Rais wa TFF, Wallace Karia (wa pili kushoyo) akiwa na viongozi wa Simba leo Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.  Kutoka kulia ni Shaaban Mnyaa mwanachama maarufu wa klabu hiyo Morogoro, Rais Evans Aveva, Wajumbe wa Kamati ya Utendaji, Musley Ruweyh na Adam Mgoyi. Kushoto kabisa ni Makamu wa Rais wa Simba, Geoffrey Nyange 'Kaburu'

    Walikuwa wameketi jukwaa kuu eneo la VIP wakishuhudia kocha Mcameroon, Joseph Marius Omog akiwafua vijana wake kwa ajili yaa mcheo dhidi ya timu yake ya zamani, Azam FGC.
    Omog amebeba kikosi chake kamili kwa ajili ya vita ya kusaka fainali ya Kombe la ASFC katika kuwania tiketi ya kucheza Kombe la Shirikisho Afrika mwakani.
    Kwa kufahamu ugumu wa mchezo huo, Simba imekiondoa kikosi chake mjini na kukipeleka Morogoro ili kuelekeza vyema akili zao kwenye mechi hiyo.
    Ikumbukwe Simba wamefungwa na Azam 1-0 mara mbili mfululizo mwezi Janauri, kwanza tarehe 13 katika fainali ya Kombe la Mapinduzi bao pekee la Himid Mao dakika ya 12 Uwanja wa Amaan, Zanzibar na baadaye tarehe 28 katika mchezo wa marudiano wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara bao pekee la Nahodha John Raphael Bocco ‘Adebayor’ Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Na hiyo ilifuatia Simba kuifunga Azam FC 1-0 katika mchezo wa Ligi Kuu mzunguko wa kwanza Uwanja wa Taifa, bao pekee la winga Shiza Ramadhani Kichuya dakika ya 67.
    Maana yake Jumamosi itakuwa inawania kuweka rekodi ya kufungana sawa kwa msimu huu na Azam FC.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAKAMU WA RAIS TFF AHUDHURIA MAZOEZI YA SIMBA MOROGORO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top