• HABARI MPYA

    Sunday, September 25, 2016

    STARS WAIFUATA ETHIOPIA MECHI YA KIRAFIKI OKTOBA 8

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars inatarajiwa kucheza na Ethiopia katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa Oktoba 8, 2016 mjini Addis Ababa.
    Mchezo huo ulio katika kalenda ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), umeombwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu la Ethiopia (EFF).
    Lakini ni faida kwa Tanzania kama itashinda mchezo huo kwa maana kina alama za nyongeza kama inatokea unaifunga timu mwenyeji.
    Kiungo wa Tanzania, Farid Mussa (akimtoka) kiungo wa Misri, Mohammed El Nenny katika mchezo uliopita wa Taifa Stars
    Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Charles Boniface Mkwasa atakuwa na nafasi ya kuandaa kikosi chake kuanzia Oktoba 3, 2016 mara baada ya michezo ya Ligi Kuu Tanzania Bara ambako Mwadui itacheza na Azam huku Mbao ikishindina na JKT Ruvu Oktoba 2, mwaka huu kabla ya kupisha kalenda hiyo ya FIFA.
    Matokeo ya mchezo huo, ni sehemu malumu kupima viwango vya ubora na uwezo wa timu za taifa. Kwa sasa Tanzania inashika nafasi ya 132 kati ya nchi 205 wanachama wa FIFA zilizopimwa ubora. Ethiopia yenyewe inashika nafasi ya 126.
    Argentina inaongoza ikifuatiwa na Ubelgiji anakocheza Mbwana Samatta – nyota wa kimataifa wa Tanzania. Samatta anacheza klabu ya K.R.C Genk inayoshiriki Ligi Kuu ya Ubelgiji. Timu nyingine bora kimataifa ni Ujerumani, Colombia na Brazil.
    Katika Bara la Afrika, Ivory Coast ambayo ni ya 34 kwa ubora duniani ndiyo inayoongoza ikifuatiwa na Algeria, Senegal, Tunisia na Ghana.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: STARS WAIFUATA ETHIOPIA MECHI YA KIRAFIKI OKTOBA 8 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top