• HABARI MPYA

    Monday, September 12, 2016

    MSUVA: REFA ALIAMUA TU KUNINYIMA BAO LA 50 YANGA, ILA HAINA NOMA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    WINGA wa Yanga SC, Simon Happygod Msuva amesema kwamba refa wa mchezo wa Jumamosi kati yao na Maji Maji FC, Emmanuel Mwandembwa wa Arusha aliamua tu kumnyima bao siku hiyo.
    Msuva amelalamikia refa huyo kumuamuru kurudia penalti hadi akakosa Jumamosi, Yanga SC ikishinda 3-0 dhidi ya Majimaji.
    Mwandembwa aliwapa Yanga penalti, baada ya mwenyewe Msuva kuangushwa – lakini mfungaji huyo bora wa Ligi Kuu msimu wa 2014- 2015 akafunga mara mbili mfululizo, zote refa huyo wa Arusha akikataa kabla ya kwenda kugongesha mwamba mkwaju wa tatu.
    Simon Msuva akipiga penalti ya kwanza ambayo alifunga, lakini refa akakataa

    Bahati nzuri, Deus David Kaseke akamalizia mpira uliorudi kuipatia Yanga bao la kwanza kipindi cha kwanza na Mrundi, Amissi Tambwe akafunga mawili kipindi cha pili kukamilisha ushindi wa 3-0. 
    “Nilikwenda kupiga ya kwanza kwa kujiamini kabisa na nikafuga, refa akasema nilitishia nirudie. Na nilikwenda kurudia kwa kujiamini pia na nikafunga tena. Refa akasema sijui wachezaji wenzangu walisogea, nirudie. Pale akanivunja nguvu ndiyo maana hata nikakosa,”alisema Msuva.
    Msuva alisema kwamba hata kipa angekuwa mbovu kiasi gani, lakini ni vigumu kutookoa japo penalti moja kati ya tatu.
    Simon Msuva alikwenda kushangilia baada ya kufunga penalti ya pili pia, lakini refa akamtaka kurudia tena
    Simon Msuva akapiga penalti kwa mara ya tatu, lakini hakuweza kufunga 
    Mkwaju wake uligonga mwamba na kurudi uwanjani, kabla ya Deus Kaseke kuifungia Yanga bao la kwanza 

    “Lakini si mbaya, sikufunga ila timu ilishinda na hilo ndilo kubwa. Ninamshukuru Mungu tulishinda na tunaendelea na vita ya ubingwa,”alisema.
    Kama angefunga mwishoni mwa wiki, Msuva angefikisha mabao 50 katika mechi 160 alizoichezea Yanga tangu ajiunge nayo mwaka 2012 akitokea Moro United. 
    Msuva sasa atajaribu kulisaka bao la 50 katika mechi yake ya 161 Jumamosi ijayo Yanga SC itakapomenyana na wenyeji Mwadui FC Uwanja wa Kambarage, Shinyanga.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MSUVA: REFA ALIAMUA TU KUNINYIMA BAO LA 50 YANGA, ILA HAINA NOMA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top