• HABARI MPYA

    Monday, May 23, 2016

    NKONGO KUCHEZESHA YANGA NA AZAM KESHOKUTWA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    REFA mahiri nchini, Israel Mujuni Nkongo wa Dar es Salaam, Jumatano Mei 25, 2016 ameteuliwa kuwa mwamuzi atakayechezesha mchezo wa fainali za Kombe la Shirikisho maarufu kama Azam Sports Federation Cup (ASFC) itakayozikutanisha timu za Young Africans, maarufu Yanga SC na Azam FC zote za Dar es Salaam.
    Mchezo huo utakaoanza kesho saa 10.30 jioni kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam waamuzi wasaidizi watakuwa Ferdinand Chancha wa Mwanza (line 1) na upande wa pili ni Soud Lila wa Dar es Salaam (line 2) na mwamuzi wa akiba mezani ni Frank Komba wa Dar es Salaam pia. Kamishna wa mchezo huo anatakuwa Juma Mgunda wa Tanga.
    Israel Mujuni Nkongo (kulia) atachezesha mechi ya fainali ya Kombe la ASFC

    Kwa mujibu wa kanuni za Ligi Kuu msimu 2015/16, mabingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu 2015/16 wataiwakilisha nchi katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu wa 2016/17. Nafasi hiyo imechukuliwa na Yanga SC.
    Kadhalika Azam ina tiketi tayari ya kushiriki Kombe la Shirikisho Barani Afrika kwa kufika fainali za ASFC ingawa kanuni zinataka bingwa ambako kwa upande wa Yanga wana tiketi ya michuano ya juu zaidi ya shirikisho. Mvuto wa mchezo wa Jumatano ni ushindani wa soka na zawadi kwa bingwa.
    Fainali za Kombe la Shirikisho zinakuja baada ya mchuano ulioshindanisha timu 64 za Ligi Kuu Tanzania Bara - VPL (16); Ligi Daraja la Kwanza -FDL (24), Ligi Daraja la Pili – SDL (24).Wakati huo huo: Kamati ya Waamuzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limeteua waamuzi 40 watakaochezesha Ligi ya Mabingwa Mikoa (RCL) inayoanza leo Mei 23 katika vituo vinne tofauti hapa nchini.
    Ligi hiyo inayoshirikisha timu 27, imegawanywa katika makundi manne ambako bingwa katika kila kundi atapanda daraja hadi Ligi Daraja la Pili msimu wa 2016/17 ngazi ya taifa kabla ya kutafuta nafasi ya kucheza Ligi daraja la Kwanza msimu wa 2017/18.
    Timu tano zitapanda daraja hadi Ligi Daraja la Pili ambako mbali ya washindi katika vituo vyote vinne, mshindwa bora katika vituo vya Njombe, Morogoro na Singida nayo itapanda daraja kwa kuangalia vigezo vya wingi wa pointi, wastani wa mabao, mabao kufunga na mabao ya kufungwa. Kituo cha Kagera hakijajumuishwa kwa kuwa kina timu shiriki sita.
    Waamuzi walioteuliwa kuchezesha ligi hiyo kwa kituo cha Njombe ni Elasto Msaliwa, Klement Manga, Mashaka Lulambo, Lazaro Mbogoro, Michael Mkongwa, Alex Chitalula, Maulid Makiwa, Michael Kilango, Edina Ndelwa na Haidal Kisingile.
    Timu zinazoshiriki ni Mkali Stars ya Ruvuma, Mtwivila (Iringa), Sido FC (Mbeya), Jangwani FC ya Rukwa, Nyundo FC ya Katavi, Mawezi ya Morogoro na Zimamoto ya Ilala, Dar es Salaam.
    Kituo cha Morogoro walioteuliwa ni Athuman Lazi, Mohammed Theophil, Seleman Kinugane, Fikiri Yusuph ‘Magari’, Nicolaus Makangara, Mwarabu Mumba, Emmanuel Muga, Herry Shao, Shaban Juma na Makongo Katuma na timu zinazoshiriki ni Stend  FC ya Pwani, Mbuga FC (Mtwara), Namungo FC(Lindi), Muheza United ya Tanga, Stand Misuna FC ya Singida, Makumbusho ya Kinondoni na Sifa Politan SC ya Temeke, Dar es Salaam.
    Kituo cha Singida wako Meshack Suda, Abdallah Mwinyimkuu, Sarah Bongi, Lucas Mathias, Amani Mwaipaja, Siyachitema Kawinga, Theophil Tegamaisho, Shaaban Msangi, Aboubakar Irume na Frederick Ndahani na timu shiriki ni Veyula FC (Dodoma), Pepsi SC (Arusha), Kitayosce FC (Kilimanjaro), Stand FC (Tabora), Murusagamba FC (Kagera), Fire Stone (Manyara) na Tomato FC (Njombe).
    Kituo cha Kagera walioteuliwa ni Jonesia Rukyaa, Jamada Ahmada, Ringston Rwiza, Grayson Buchard, Grace Wamala, Edgar Lyombo, Yahaya Juma, Adrian Karisa, Getrude Kahawa na Ahmada Simba na timu shiriki ni Geita Town Council Fc (Geita), Gold Sports Academy (Mwanza), Kabela City (Shinyanga), Ambassador FC (Simiyu), Igwe FC (Mara) na Mashujaa (Kigoma).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NKONGO KUCHEZESHA YANGA NA AZAM KESHOKUTWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top