• HABARI MPYA

    Sunday, May 29, 2016

    YANGA KUWEKA KAMBI UTURUKI KUJIANDAA NA WAALGERIA KOMBE LA SHIRIKISHO

    Na Somoe Ng’itu, DAR ES SALAAM
    YANGA SC itaweka kambi Uturuki kabla ya kwenda Algeria kumenyana na MO Bejaia katika mchezo wa kwanza wa Kundi A Kombe la Shirikisho Afrika Juni 17, mwaka huu.
    Kikao cha Kamati ya Mashindano ya Yanga kilichofanyika juzi jioni mjini Dar es Salaam kikimuhusisha Kocha Mkuu, Mholanzi, Hans van der Pluijm kimeamua timu iweke kambi nje ya nchi kabla ya mchezo huo.
    Na wachezaji wamepewa mapumziko ya siku tano hadi Jumatatu watakapokutana tena kuanza mazoezi, wakiungana na wenzao waliokwenda kuzitumikia timu zao za taifa.
    Wachezaji wa Yanga waliokwenda kuzitumikia timu za taifa ni Vincent Bossou wa Togo, Haruna Niyonzima wa Rwanda na Watanzania, Deo Munishi ‘Dida’, Juma Abdul, Mwinyi Hajji Mngwali na Deus Kaseke.
    Yanga wakiwa kambini Uturuki mwaka 2013 chini ya kocha Ernie Brandts

    Hao wataungana na waliobaki, Ally Mustafa ‘Barthez’, Benedicto Tinocco, Mbuyu Twite, Kevin Yondan, Pato Ngonyani, Nahodha Nadir Haroub 'Cannavaro', Thabani Kamusoko, Salum Telela, Simon Msuva, Said Juma, Issoufou Boubacar, Godfrey Mwashiuya, Donald Ngoma, Matheo Anthony, Amissi Tambwe, Malimi Busungu na Paul Nonga.
    Mbali na Yanga na MO Bejaia, timu nyingine katika Kundi la A ni TP Mazembe ya DRC na Medeama ya Ghana, wakati 
    Kundi B linaundwa na timu za Kaskazini mwa Afrika tupu ambazo ni Etoile du Sahel ya Tunisia ambao ni mabingwa watetezi, Ahly Tripoli ya Libya, FUS Rabat na Kawkab zote za Morocco.
    Yanga itafungua dimba na Mouloudia Olympique Bejaia nchini Algeria Juni 17, mwaka huu siku ambayo, mabingwa wa zamani wa Afrika, TP Mazembe ya DRC watakuwa wenyeji wa Medeama ya Ghana katika mchezo mwingine wa kundi hilo.
    Mechi za Kundi B siku hiyo; Kawkab Marakech watakuwa wenyeji wa mabingwa watetezi Etoile du Sahel katika mchezo wa Kundi B nchini Morocco, wakati F.U.S Rabat watakuwa wenyeji wa Ahly Tripoli nchini Morocco pia.
    Ikitoka Algeria, Yanga itarejea nyumbani kuikaribisha TP Mazembe Juni 28, kabla ya kumaliza na Medeama ya Ghana Julai 15, Dar es Salaam pia katika mechi za mzunguko wa kwanza.
    Mzunguko wa pili, Yanga itaanzia Ghana dhidi ya Medeama Julai 26, kabla ya kurudi nyumbani nyumbani tena na MO Bejaia Agosti 12 na kasha kwenda kumalizia Lubumbashi dhidi ya TP Mazembe Agosti 23.
    Yanga imekwishawahi kuweka kambi mara mbili Uturuki, kwanza mwaka 2013 chini ya kocha Mholanzi pia, Ernie Brandts na mwaka 2014 ikiwa chini ya Charles Boniface Mkwasa ambaye baadaye alimpokea Pluijm alipoajiriwa kwa mara ya kwanza.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA KUWEKA KAMBI UTURUKI KUJIANDAA NA WAALGERIA KOMBE LA SHIRIKISHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top