• HABARI MPYA

    Tuesday, May 24, 2016

    YANGA YAPANGWA NA MAZEMBE, MEDEAMA NA WAALGERIA KOMBE LA SHIRIKISHO

    YANGA SC imepangwa kundi la A katika Kombe la Shirikisho Afrika pamoja na mabingw awa zamani barani, TP Mazembe ya DRC, MO Bejaia ya Algeria na Medeama ya Ghana.
    Kundi B linaundwa na timu za Kaskazini mwa Afrika tupu ambazo ni Etoile du Sahel ya Tunisia ambao ni mabingwa watetezi, Ahly Tripoli ya Libya, FUS Rabat na Kawkab zote za Morocco.
    Mechi za mzunguko wa kwanza zitachezwa Juni 17, mwaka huu na Ratiba hiyo inamaanisha Yanga itakutana na timu ya mshambuliaji wa Tanzania, Thomas Ulimwengu wa TP Mazembe ya DRC.


    Yanga SC imepangwa kundi moja na TP Mazembe ya DRC katika Kombe la Shirikisho Afrika

    Na mkutano huo ni kutimia kwa ndoto za Ulimwengu, ambaye wiki iliyopita alikakaririwa na BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE akisema ana hamu ya kupanga na Yanga.
    Ulimwengu alisema anatamani katika droo ya CAF wapangwe na Yanga na atafurahi kucheza dhidi ya timu ya nyumbani. “Itakuwa mechi nzuri sana sisi na Yanga, yaani mimi nacheza pale Taifa dhidi ya Yanga, tamu sana,”alisema Uli maarufu kwa jina la Rambo mjini Lubumbashi.
    Na mapema leo, kiungo wa kimataifa wa Rwanda, Haruna Niyonzima anayechezea Yanga amesema kwamba sasa wana uzoefu wa kutosha wa mashindano makubwa baada ya kucheza mfululizo, hivyo hawaihofii timu yoyote watakayopangwa nayo.

    “Katika kipindi cha miaka hii mitatu tumecheza na timu za Kaskazini mwa Afrika, Kusini na huku kwetu Mashariki, bahati mbaya hatujakutana na timu za Magharibi ambazo kwa sasa si tishio,”amesema Niyonzima.
    Nahodha huyo wa Amavubi amesema kwamba katika kundi lolote watakaloangukia watapambana wafanye vizuri ili wafike mbali.
    Katika Ligi ya Mabingwa Afrika kundi A kuna timu za Zesco United ya Zambia, Al Ahly ya Misri, Asec Mimosa ya Ivory Coast, Waydad Casablanca ya Morocco, wakati Kundi B kuna Enyimba ya Nigeria, Zamalek ya Misri, ES Setif ya Algeria na Mamelodi Sundown ya Afrika Kusini. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA YAPANGWA NA MAZEMBE, MEDEAMA NA WAALGERIA KOMBE LA SHIRIKISHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top