• HABARI MPYA

    Sunday, April 03, 2016

    YANGA OYEEE OYEEE, KAGERA AFA 3-1 TAIFA, AZAM 1-1 NA TOTO KIRUMBA

    Na Prince Akbar, DAR ES SAALM
    YANGA SC imejiweka katika nafasi nzuri ya kutetea ubingwa wake wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kufuatia ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Kagera Sugar ya Bukoba jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. 
    Ushindi huo, unaifanya Yanga SC ifikishe pointi 53 baada ya kucheza mechi 22, nyuma ya Simba SC yenye pointi 57 za mechi 24 ikifuatiwa na Azam FC yenye pointi 51 za mechi 22 pia.
    Hadi mapumziko, timu hizo zilikuwa zimekwishafungana bao 1-1, Kagera Sugar wakitangulia kupitia kwa mshambuliaji chipukizi, Mbaraka Yussuf dakika ya tisa, akimalizia krosi ya beki wa kulia, Salum Kanoni.
    Mfungaji wa bao la pili la Yanga leo, Amissi Tambwe (mbele) akishangilia na mfungaji wa bao la kwanza, Donald Ngoma (nyuma kulia)
    Hata hivyo, Yanga SC ilifanikiwa kusawazisha bao hilo kupitia kwa mshambuliaji wake kutoka Zimbabwe, Donald Ngoma aliyemalizia kwa kichwa krosi ya beki wa kulia, Juma Abdul dakika ya 26.
    Yanga ingeweza kwenda kupumzika ikiwa inaongoza kama si beki wake Kevin Yondan kumdakisha penalti kipa wa Kagera, Andrew Ntalla dakika ya 35, baada ya Ngoma kuangushwa na Shaaban Ibrahim ndani ya boksi.
    Kipindi cha pili, Yanga walirudi kwa kasi nzuri, huku Kagera wakionekana kucheza kwa kujihami zaidi.
    Kagera ilimpoteza beki wake, Shaaban Ibrahim aliyetolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 47 baada ya kuonyeshwa kadi ya pili ya njano na refa Erick Unoka wa Arusha kwa kumchezea rafu Ngoma. 
    Kipa Andrew Ntalla alimtemea mpira kiungo Salum Telela ndani ya boksi dakika ya 55, lakini kwa mastaajabu ya wengi kiungo wa Yanga akapiga nje.
    Mshambuliaji kutoka Burundi, Amissi Tambwe akaifungia  Yanga bao la ushindi dakika ya 62 kwa shuti la mguu wa kulia akimalizia pasi ya mfungaji bora wa Ligi Kuu msimu uliopita, Simon Msuva.
    Beki wa kushoto, Mwinyi Hajji Mngwali aliifungia Yanga SC bao la tatu dakika ya 89 akimalizia kona ya Msuva.
    Mchezo mwingine wa Ligi Kuu leo, Azam FC imelazimishwa sare ya 1-1 na wenyeji Toto Africans Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.
    Azam FC ndiyo waliotangulia kupata bao kupitia kwa Nahodha wake, John Raphael Bocco dakika  ya 23, kwa kichwa akimalizia krosi ya Khamis Mcha ‘Vialli’, kabla ya Toto kusawazisha kupitia kwa Waziri Juma dakika ya 40.
    Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul/Pato Ngonyani dk90+1, Mwinyi Hajji, Vincent Bossou, Kevin Yondan, Salum Telela, Simon Msuva, Thabani Kamusoko, Donald Ngoma, Amissi Tambwe/Paul Nonga dk79 na Deus Kaseke/Godfrey Mwashiuya dk60.
    Kagera Sugar; Andrew Ntalla, Salum Kanoni, Juma Jabu, Erick Kuaruzi, Shaaban Ibrahim, George Kavilla, Daud Jumanne, Babu Ally, Mbaraka Yussuf/Ramadhani Kipalamoto dk74, Martin Lupert/Job Ibrahim dk51 na Paul Ngway/Iddi Kulachi dk57.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA OYEEE OYEEE, KAGERA AFA 3-1 TAIFA, AZAM 1-1 NA TOTO KIRUMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top