• HABARI MPYA

    Wednesday, October 07, 2015

    YANGA SC WAANZA MAZUNGUMZO NA PLUIJM JUU YA MKATABA MPYA, APEWA UHURU WA KUCHAGUA MBADALA WA MKWASA JANGWANI

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    YANGA SC wanatarajiwa kuanza mazungumzo na kocha wao, Mholanzi Hans van der Pluijm juu ya Mkataba mpya, wakati ule uliomo kabatini unamalizika Desemba.
    Na Yanga SC baada ya kumuacha aliyekuwa Msaidizi wa Mholanzi huyo, Charles Boniface Mkwasa ahamie Taifa Stars- imempa Pluijm jukumu la kuchagua Msaidizi mwingine, ingawa Freddy Felix Minziro ‘anapigiwa chapuo’.
    Minziro aliyejiuzulu kutokana na matokeo mabaya JKT Ruvu, ni kipenzi cha wana Yanga SC akiwa mchezaji na kocha wa zamani wa timu hiyo.
    Katibu Mkuu wa Yanga SC, Dk. Jonas Tiboroha ameiambia BIN ZUBEIRY SPORTS- ONLINE jana kwamba, wanatarajiwa kuanza mazungumzo na Pluijm muda si mrefu.
    Pluijm (kulia) akiwa na Mkwasa, ambaye sasa anakuwa kocha wa kudumu wa Taifa Stars

    “Pluijm Mkataba wake wa sasa unamalizika Desemba, kwa hivyo muda si mrefu tutaanza mazungumzo naye juu ya Mkataba mpya,”amesema Dk. Tiboroha. 
    Pluijm amefanya kazi kwa awamu mbili hadi sasa Yanga SC, kwanza kuanzia Januari 2014 akirithi mikoba ya Mholanzi mwenzake, Ernie Brandts hadi Juni alipokwenda kufundisha Al Shoalah FC ya Saudi Arabia.
    Yanga SC ilimuajiri Mbrazil Maximo, ambaye baada ya miezi mitano akafukuzwa kufuatia kipigo cha mabao 2-0 kutoka kwa Simba SC Desemba 13, mwaka jana katika mchezo wa Nani Mtani Jembe 2, mabao ya Awadh Juma na Elias Maguri. 
    Hans van der Pluijm akarudishwa Jangwani Januari mwaka huu, akimalizia vizuri msimu kuwa kuiwezesha Yanga SC kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na kuifikisha timu hatua ya 16 Bora Kombe la Shirikisho Afrika ambako ilitolewa na Etoile du Sahel ya Tunisia.
    Katika kipindi chake cha awali, Pluijm aliiongoza Yanga SC katika mechi 19, akishinda 11, sare sita na kufungwa mbili, moja tu nyumbani 2-1 mbele ya Mgambo JKT mjini Tanga, nyingine akifungwa na Al Ahly 1-0 katika Ligi ya Mabingwa Afrika mjini Alexandria Misri. 
    Na aliporejea Januari mwaka huu, hadi sasa ameiongoza Yanga SC katika mechi 46 za mashindano yote, akishinda 31, sare saba na kufungwa nane. Kwa ujumla Pluijm ameiongoza Yanga SC katika mechi 65, akishinda 42, sare 13 na kufungwa 10. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC WAANZA MAZUNGUMZO NA PLUIJM JUU YA MKATABA MPYA, APEWA UHURU WA KUCHAGUA MBADALA WA MKWASA JANGWANI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top