• HABARI MPYA

    Saturday, October 17, 2015

    AMANI YANUKIA SOKA YA ZANZIBAR, WALIOKWENDA MAHAKAMANI WAKUBALI KUFUTA KESI

    Rais wa ZFA, Ravia Idarous
    Na Ameir Khalid, ZANZIBAR
    JITIHADA za kuurejeshea utulivu mchezo wa soka Zanzibar zimeanza kuzaa matunda baada ya klabu za Chuoni SC na Aluta SC kukubali kufuta kesi walizofungua mahakama ya mkoa Vuga dhidi ya Chama cha Soka Zanzibar (ZFA).
    Awali Chuoni ilikuwa imefungua kesi ikiilaamikia ZFA kwa kukiuka kanuni kwa kutoirudisha Ligi Kuu ya Zanzibar baada ya kushuka msimu uliopita, huku Aluta ilichukua hatua kama hiyo ikidai imenyimwa kwa njama za makusudi nafasi ya kucheza daraja la pili Taifa.
    Akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa uwanja wa Amaan jana, Katibu wa kamati hiyo Hashim Salum, alisema juzi kamati ilifanya kikao na viongozi wa timu zote mbili na kusikiliza kutoka kwao sababu za msingi zilizowafanya wafungue kesi hizo.
    Hashim alisema Katibu wa Aluta Shaaban Sariboko Makarani, na meneja msaidizi wa Chuoni Bakari Hussein, wote kwa pamoja wameridhia ushauri wa kufuta kesi hizo ili kutoa nafasi mpira urejee viwanjani.
    Aidha alisema, hatua hiyo pia itainufaisha klabu ya Shaba SC kurudi Ligi Kuu ya soka Zanzibar baada ya kushuka daraja pamoja na Chuoni.
    Hashim alisema taratibu za kutekeleza matakwa ya kisheria ili kesi hizo ziweze kuondolewa mahakamani zilikuwa zikiendelea jana kwa kushirikisha mawakili wa wadai hao, zikitarajiwa hadi leo mchana ziwe zimekamilika.
    Kwa hivyo alisema, kufuatia mafanikio hayo ya awali, kamati hiyo inaandaa utaratibu ili Ligi Kuu ya Zanzibar iweze kuanza wakati wowote kati ya Novemba 5 na 10 mwaka huu.
    Katika hatua nyengine, Katibu huyo alisema wajumbe wawili wa kamati hiyo wanaondoka keshokutwa Jumatatu kwenda jijini Dar es Salaam kukutana na uongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa ajili ya kulijulisha mabadiliko yaliyofikiwa hadi sasa.
    Wajumbe hao ni Masoud Attai na Hashim Salum mwenyewe.   
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AMANI YANUKIA SOKA YA ZANZIBAR, WALIOKWENDA MAHAKAMANI WAKUBALI KUFUTA KESI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top