• HABARI MPYA

    Monday, October 26, 2015

    MAVUGO ATUMA HABARI NJEMA SIMBA SC; “NAMALIZA MKATABA JANUARI VITAL'O, NAWEZA KUJA KWENU”

    Na Harakandi Patrick, BUJUMBURA
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Burundi, Laudit Mavugo (pichani) amesema kwamba anaweza kujiunga na Simba SC ya Tanzania mwakani, baada ya kumaliza Mkataba wake Vital’O ya kwao.
    Simba SC ilikaribia kumsajili Mavugo Julai mwaka huu, kama si kushindwa dau kubwa la klabu yake na kuamua kuachana naye.
    Hata hivyo, mkali huyo wa mabao wa Burundi amewapa moyo Simba SC baada ya kusema kwamba anaweza kujiunga na klabu hiyo atakapomaliza Mkataba wake.
    “Ninaweza kuondoka hapa baada ya Januari, nitakuwa nimemaliza Mkataba wangu Vital’O. kama Simba watakuwa bado wananihitaji tutajua wakati ukifika,”alisema.
    Mavugo alitarajia kupandisha soko lake iwapo Burundi ingefuzu michuano ya CHAN inayofanyika Rwanda mapema mwakani, lakini baada ya kutolewa na Ethiopia jana amekata tamaa.
    Simba SC ilitoa tamko la kuachana na Mavugo mapema Agosti ikilalamika klabu mbili za Burundi kupandisha thamani ya mchezaji huyo na kuwa Sh. Milioni 200, badala 110 zilizokubakiwa awali.
    Rais wa Simba SC, Evans Elieza Aveva alisema pamoja na jitihada za kutuma viongozi Bujumbura kwa mijadala mirefu suala hilo lilishindikana.
    Aveva amesema walikubaliana mchezaji asajiliwe kwa Sh 110 milioni baada ya michuano ya Ligi Kuu na Kombe la FA Burundi na Simba SC ilimtuma Makamu wake wa Rais, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ aende Bujumbura kukamilisha majadiliano na uongozi wa Vital’O juu ya usajili wa Laudit Mavugo. 
    Alisema lakini ajabu, Vital’O wakabadilika na kuongeza maradufu thamani ya mchezaji huyo pamoja na vipengele vipya vya mauzo kinyume na makubaliano ya awali.
    Alisema kuliibuka pia mzozo mpya kati ya klabu ya Vital’O FC na Solidarity FC, inayodai kumlea Mavugo, hivyo nayo kudai ina hakimiliki ya mchezaji huyo.
    “Licha ya mkanganyiko wa umiliki wake, Vital’O imedai kuwepo kipengele kipya kinachodai mapato ya asilimia 50 kama mchezaji huyo atauzwa na Simba SC kwenda klabu nyingine,”amesema.
    (Harakandi Patrick ni Mtangazaji wa Redio ya Taifa Burundi)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAVUGO ATUMA HABARI NJEMA SIMBA SC; “NAMALIZA MKATABA JANUARI VITAL'O, NAWEZA KUJA KWENU” Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top