• HABARI MPYA

    Tuesday, October 20, 2015

    MALIMI BUSUNGU: KESHO HATURUDII MAKOSA

    Malimi Busungu amesema hawataki kurudia makosa katika mchezo wa kesho na Toto Africans

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa Yanga SC, Malimi Busungu amesema kwamba walishindwa kutumia nafasi nyingi walizotengeneza katika mchezo uliopita wakitoa sare na Azam FC na hawataki kurudia makosa katika mchezo ujao na Toto Africans.
    Baada ya sare ya 1-1 na Azam FC Jumamosi, Yanga SC wanashuka tena dimbani kesho Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam katika mfululizo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kumenyana na Toto.
    Na akizungumza na BIN ZUBEIRY SPORTS- ONLINE jana, Busungu amesema kwamba wanajutia makosa waliyoyafanya katika mchezo uliopita, lakini wanasonga mbele.
    “Hii ni Ligi, kila timu ni ngumu, kwa hivyo hatuwezi kusema Toto tutawafunga kwa urahisi. Utakuwa mchezo mgumu pia, lakini tutajitahidi tusirudie makosa,”amesema.
    Busungu amewaomba mashabiki wa Yanga SC kuendelea kujitokeza kwa wingi uwanjani kuisapoti timu yao na watarajie matokeo mazuri.
    “Kwa kiasi fulani tunajua tuliwaangusha mashabiki wetu, lakini hayo mambo yanatokea katika michezo, ila tunawaahidi kesho hatutarudia makosa,”.
    Kwa ujumla, Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inatarajiwa kuendelea kesho na mbali na Yanga SC na Toto Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Stand United na Majimaji FC Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga, JKT Ruvu na Mtibwa Sugar Uwanja wa Karume, Dar es Salaam, Prisons na Simba SC Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya na Coastal Union na Kagera Sugar Uwanja wa Mkwakwani, Tanga Jumatano.
    Ligi Kuu itaendelea tena Alhamisi, Ndanda FC wakiwa wenyeji wa Azam FC Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara, Mwadui FC ikimenyana na Mgambo Shooting Uwanja wa Mwadui Complex, Shinyanga wakati Mbeya City watakuwa wenyeji wa African Sports ya Tanga.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MALIMI BUSUNGU: KESHO HATURUDII MAKOSA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top