• HABARI MPYA

    Wednesday, October 21, 2015

    YANGA SC YALIPIGA 4-1 TOTO LAKE NA KUTANUA MABEGA KILELENI

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    YANGA SC imejiweka vizuri katika kiti cha usukani wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya kuichapa mabao 4-1 Toto Africans ya Mwanza jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. 
    Ushindi huo unaifanya Yanga SC ifikishe pointi 19 baada ya mechi saba, ikiwazidi kwa pointi tatu Azam FC ambao kesho wanacheza mechi ya saba dhidi ya Ndanda FC mjini Mtwara. 
    Hadi mapumziko, Yanga SC walikuwa mbele kwa bao 1-0 lililofungwa na beki wa kulia, Juma Abdul dakika ya tisa kwa shuti kali umbali wa zaidi ya mita 20 akimaizia kona ya Haruna Niyonzima.
    Mfungaji wa mabao mawili ya Yanga SC, Simon Msuva (kushoto) akiwakimbilia wenzake kushangilia nao
    Kikosi cha Yanga SC kilichoanza leo

    Hata hivyo, Yanga SC wangeweza kumaliza dakika 45 za kwanza wakiwa wanaongoza kwa mabao zaidi kama wangetumia vizuri nafasi zote walizotengeneza, ikiwemo penalti ambayo alikosa Mzimbabwe Donald Ngoma.
    Ngoma alikosa penalti hiyo dakika ya 45 ikipanguliwa na kipa wa Toto, Mussa Mohammed baada ya yeye mwenyewe kumnawisha mpira beki Carlos Protas na refa Ahmada Simba wa Kagera akaamuru pigo hilo.
    Katika kipindi cha kwanza, Toto walifanya shambulizi moja tu la maana, Miraji Athumani ‘Madenge’ akishindwa kumalizia vizuri pasi ya Edward Christopher dakika ya 42 kwa kumpa nafasi kipa wa Yanga SC, Ally Mustafa ‘Barthez’ kupangua.
    Kipindi cha pili, Yanga SC walianza na mabadiliko Juma Abdul akimpisha Simon Msuva ambaye alikwenda kufunga bao la pili dakika ya 49.
    Kiungo Haruna Niyonzima wa Yanga SC akimtoka beki wa Toto, Hassan Khatib 

    Toto Africans ilipata bao lake dakika ya 62 kupitia kwa Miraj Athumani ‘Madenge’ kwa kichwa akimalizia mpira ulioparazwa na kipa Ally Mustafa ‘Barthez’ baada ya mpira wa adhabu uliopigwa na Bernad Evarigetus.
    Mrundi Amissi Tambwe aliipatia Yanga SC bao la tatu dakika ya 81 akimalizia krosi ya Simon Msuva ambaye alifunga bao la nne dakika ya 90 akimalizia pasi ya Mbrazil Andrey Coutinho.
    Beki wa Toto, Hassan Khatib alionyeshwa kadi ya pili ya njano dakika ya 90 na ushei kwa utovu wa nidhamu na kutolewa kwa kadi nyekundu.
    Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul/Simon Msuva dk46, Mwinyi Mngwali, Kevin Yondan/Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Vincent Bossou, Thabani Kamusoko, Donald Ngoma, Amissi Tambwe, Malimi Busungu na Godfrey Mwashiuya/Andrey Coutinho.  
    Toto Africans; Mussa Mohammed, Hassan Khatib, Robert Magadula/Miraj Makka, Hamisi Kasanga, Carlos Protas, Salimn Hoza/William Kimanzi, Japhet Vedastus/Jaffar Mohammed, Abdallah Seseme, Evarigetus Bernad, Edward Christopher na Miraji Athumani.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YALIPIGA 4-1 TOTO LAKE NA KUTANUA MABEGA KILELENI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top