• HABARI MPYA

    Wednesday, October 21, 2015

    ARSENAL YAIKALISHA BAYERN MUNICH EMIRATES, BARCA MOTO ULE ULE, CHELSEA YAKATALIWA

    MATOKEO LIGI YA MABINGWA ULAYA JANA
    FC Porto 2 - 0 Maccabi Tel Aviv
    Dynamo Kyiv 0 - 0 Chelsea
    Valencia CF 2 - 1 KAA Gent
    Zenit St Petersburg 3 - 1 Lyon
    Bayer 04 Leverkusen 4 - 4 Roma
    BATE Borisov 0 - 2 Barcelona
    Arsenal 2 - 0 FC Bayern Munchen
    Dinamo Zagreb 0 - 1 Olympiakos
    Mesut Ozil akipiga ngumi hewani baada ya kuifungia bao la Arsenal dhidi ya Bayern Munich PICHA ZAIDI GONGA HAPA
    TIMU ya Arsenal imeichapa mabao 2-0 FC Bayern Munich usiku wa kuamkia leo katika mchezo wa Kundi F Ligi ya Mabingwa Ulaya, uliofanyika Uwanja wa Emirates, London.
    Shukrani kwao, wafungaji wa mabao hayo, Olivier Giroud dakika ya 77 na Mesut Ozil dakika ya nne ya muda wa nyongeza baada ya kutimu dakika 90 za kawaida za mchezo.
    Huo unakuwa ushindi wa kwanza kwa Arsenal katika kundi hilo baada ya kufungwa mechi mbili za awali, lakini inaendelea kushika mkia wakati Bayern Munich inaendelea kukaa kileleni.
    Mchezo mwingine wa kundi hilo, Olympiacos ya Ugiriki imeshinda 1-0 ugenini dhidi ya Dinamo Zagreb, bao pekee la Brown Ideye dakika ya 79 Uwanja wa Maksimir.
    Kiungo wa Barcelona, Ivan Rakitic (kulia) akipongezwa na mchezaji mwenzake Jordi Alba baada ya kufunga mabao mawili dhidi ya BATE Borisov PICHA ZAIDI GONGA HAPA

    Mabao mawili ya kipindi cha pili ya Ivan Rakitic dakika ya 48 na 64, yamewapa mabingwa watetezi, Barcelona ushindi wa ugenini wa 2-0 dhidi ya BATE Borisov Uwanja wa Borisov Arena katika mchezo wa Kundi E.
    Barca inaendelea kuwa kileleni mwa kundi hilo, kwa kufikisha pointi saba, tatu zaidi ya Bayer 04 Leverkusen iliyolazimishwa sare ya 4-4 na Roma jana.
    Mshambuliaji wa zamani wa Manchester United na Real Madrid, Javier Hernandez ‘Chicharito’ aliifungia mabao mawili Bayer Leverkusen, kwanza kwa penalti dakika ya nne na lingine dakika ya 19, mabao mengine yakifungwa na Kevin Kampl dakika ya 84 na Admir Mehmedi dakika ya 86.
    Mabao ya Roma yalifungwa na Daniele De Rossi dakika ya 29 na 38, Miralem Pjanic dakika ya 54 na Iago Falque dakika ya 73 Uwanja wa BayArena.
    Eden Hazard alikaribia kuifungia Chelsea jana PICHA ZAIDI GONGA HAPA
    Chelsea imepata sare ya 0-0 ugenini mbele ya Dynamo Kyiv Uwanja wa Kiev Olympic katika mchezo wa Kundi G.
    Mchezo mwingine wa kundi hilo, FC Porto wamepanda kileleni kufuatia ushindi wa 2-0 dhidi ya Maccabi Tel Aviv, mabao ya Vincent Aboubakar dakika ya 37 na Yacine Brahimi dakika ya 41 Uwanja wa Estadio do Dragao.
    Valencia CF imeshinda 2-1 dhidi ya KAA Gent katika mchezo wa Kundi H, mabao yake yakifungwa na Sofiane Feghouli dakika ya 15 na Stefan Mitrovic aliyejifunga dakika ya 72, wakati bao la wageni lilifungwa na Thomas Foket dakika ya 40 Uwanja wa Mestalla.
    Mchezo mwingine wa kundi hilo, Zenit St Petersburg imeichapa 3-1 Lyon, mabao yake yakifungwa na Artem Dzyuba dakika ya pili, Givanildo Vieira de Souza dakika ya 56 na Danny Miguel Alves Gomes dakika ya 82, huku bao pekee la wapinzani wao likifungwa na Alexandre Lacazette dakika ya 49 Uwanja wa Petrovski.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ARSENAL YAIKALISHA BAYERN MUNICH EMIRATES, BARCA MOTO ULE ULE, CHELSEA YAKATALIWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top