• HABARI MPYA

    Friday, April 06, 2018

    JKT TANZANIA KUINGIA KAMBINI LEO MAANDALIZI MECHI NA SINGIDA UNITED NUSU FAINALI ASFC

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    KIKOSI cha JKT Tanzania FC kinatarajia kuingia kambini Ijumaa kujiandaa na mchezo wake wa Nusu Fainali ya Azam Sports Federation Cup (ASFC) dhidi ya Singida United kati ya Aprili 16 na 18, mwaka huu.
    Timu hiyo iliyopanda tena Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu ujao, ilifanikiwa kuingia katika hatua hiyo baada ya kuiondoa Tanzania Prisons katika Robo Fainali iliyochezwa kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya Jumamosi iliyopita.
    Kocha Mkuu wa JKT, Bakari Shime alisema anatambua wapinzani wao hao sio wa kubeza hivyo anawatengeneza vijana wake kwa ajili ya kuhakikisha anaendeleza kiwango kile kile katika hatua hiyo ya nusu fainali.
    Kocha Mkuu wa JKT, Bakari Shime amesema anawaheshimu Singida United na atajiandaa kikamilifu kuwakabili 

    Alisema wanatarajia kwenda nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam, kwa ajili ya kuweka kambi na kufanya maandalizi yao ya kuhakikisha wanafanya vyema katika mchezo huo dhidi ya Singida. 
    “Hakuna timu ambayo nitaibeza, ukizingatia wenzetu wako katika ligi, hivyo tutakuwa makini kuhakikisha tunajiandaa vizuri,” alisema.
    Shime alisema michuano hiyo ya ASFC ni mikubwa na bingwa anawakilisha Taifa katika michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika, hivyo anaimani maandalizi mazuri yatawafikisha wanakotarajia. 
    Nusu Fainali nyingine ya Azam Sports Federation Cup itazikutanisha Mtibwa Sugar ya Morogoro na Stand United ya Shinyanga kati ya Aprili 16 na 18 pia mwaka huu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: JKT TANZANIA KUINGIA KAMBINI LEO MAANDALIZI MECHI NA SINGIDA UNITED NUSU FAINALI ASFC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top