• HABARI MPYA

    Saturday, October 14, 2017

    YANGA YAIPIGA 2-1 KAGERA SUGAR NA KUPAA KILELENI LIGI KUU

    Na Salma Suleiman, BUKOBA
    MABINGWA watetezi, Yanga SC jioni ya leo wameibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya wenyeji Kagera Sugar katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara uliofanyika Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.  
    Ushindi huo, unaifanya Yanga SC ifikishe pointi 12 baada ya kucheza mechi sita na kupanda juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu kwa wastani wa mabao, sasa wakilingana kwa pointi na Azam FC, ambayo leo imelazimishwa sare ya 1-1 na Mwadui mjini Shinyanga.
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Andrew Shamba wa Pwani, aliyesaidiwa na washika vibendera Joseph Masija na Julius Kasitu pamoja na Jamada Ahmada mezani, hadi mapumziko Yanga walikuwa mbele kwa bao 1-0.
    Ibrahim Hajib akionyesha jezi yake namba 10 baada ya kufunga bao la pli leo
    Bao hilo lilifungwa na mshambuliaji Mzambia, Obrey Chirwa dakika ya 40 aliyemhadaa beki juma Nyosso na kumchambua kipa mkongwe Juma Kaseja, kufuatia pasi nzuri ya mshambuliaji mwenza, Ibrahim Hajib ambaye naye alipasiwa na Gardiel Michael.
    Yanga wakaendelea kupeleka mashambulizi langoni mwa Kagera Sugar baada ya bao hilo, lakini Kaseja alisimama imara kuondosha hatari zote hadi filimbi ya kuugawa mchezo ilipopulizwa.
    Na mara baada ya kuanza tu kwa kipindi pili, Yanga wakafanikiwa kupata bao la pili dakika ya 47 lililofungwa na Hajib, baada ya kupewa pasi nzuri na Chirwa.
    Wakati Yanga wakiwa kwenye furaha ya kuongeza bao wakashitukizwa kwa bao la Jaffar Kibaya dakika ya 52 aliyemalizia kwa kichwa krosi ya Venence Ludovic.
    Bao hilo likazidi kuuchangamsha mchezo, Yanga wakisaka bao la tatu na Kagera Sugar wakitafuta bao la kusawazisha, lakini walikuwa ni wana Jangwani waliofanikiwa kuulinda ushindi wao wa ugenini.
    Kikosi cha Kagera Sugar kilikuwa; Juma Kaseja, Mwaita Gereza, Adeyoum Ahmed, Juma Shemvuni, Juma Nyosso, Ally Iddi, Venence Ludovic, Ozuka Okochukwu, Jaffar Kibaya, Omar Daga na Christopher Edward/Themi Felix dk64. 
    Yanga SC; Youthe Rostand, Juma Abdul, Gardiel Michael, Andrew Vincent, Kelvin Yondani, Said Juma ‘Makapu’/Raphael Daudi dk57, Pius Buswita, Papy Tshishimbi, Obrey Chirwa/Obrey Chirwa dk93, Ibrahim Hajib na Geoffrey Mwashiuya/Emmanuel Martin dk62.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA YAIPIGA 2-1 KAGERA SUGAR NA KUPAA KILELENI LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top