• HABARI MPYA

    Wednesday, October 04, 2017

    HATIMAYE NDUDA KWENDA INDIA LEO KWA MATIBABU YA GOTI

    Na Salma Suleiman, DAR ES SALAAM
    KIPA namba mbili wa Simba, Said Mohamed ‘Nduda’, anatarajiwa kuondoka leo mchana mjini Dar es Salaam kwenda India kwa ajili ya matibabu ya goti.
    Nduda aliyesajiliwa Simba Julai mwaka huu akitokea Mtibwa Sugar ya Morogoro, hajacheza mechi yoyote ya Ligi Kuu msimu huu kutokana na maumivu ya goti aliyoyapata Agosti mazoezini.
    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online leo mjini Dar es Salaam, Nduda alisema tayari kila kitu kimekamilika juu ya safari yake na anatarajiwa kuondoka mchana wa leo kwenda India kwa matibabu.
    Said Mohamed ‘Nduda’, anaondoka leo mchana kwenda India kwa matibabu ya goti

    “Kila kitu kimekamilika na natarajia kuondoka leo mchana kwenda nchini India kwa ajili ya matibabu,” alisema Nduda, aliyewahi pia kudakia Maji Maji ya Songea na Yanga ya Dar es Salaam kabla ya kwenda Mtibwa.
    Simba ilivutiwa na Nduda na kumsajili baada ya kudaka vizuri katika mchezo wa kusaka mshindi wa tatu wa Kombe la COSAFA dhidi ya Lesotho Julai 7, mwaka huu mjini Rusternburg, Afrika Kusini Taifa Stars ikishinda kwa penalti baada ya sare ya 0-0. 
    Na Nduda akashinda tuzo ya kipa bora wa mashindano hayo baada ya kazi yake nzuri kwenye mchezo huo mmoja tu, kiasi cha kuwashawishi na Simba kumsajili na kumuunganisha na kipa namba wa Taifa Stars, Aishi Manula.
    Wakati huu Ndunda anasumbuliwa na maumivu ya goti, kocha wa Taifa Stars, Salum Shaaban Mayanga amewaita Manula, Peter Manyika wa Singida United na Ramadhani Kabwili wa Yanga. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HATIMAYE NDUDA KWENDA INDIA LEO KWA MATIBABU YA GOTI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top