• HABARI MPYA

    Tuesday, March 01, 2016

    ISIHAKA AOMBA RADHI SIMBA, MAYANJA ASEMA ALISTAHILI ADHABU

    Na Somoe Ng’itu, DAR ES SALAAM
    BEKI Hassan Isihaka ameomba radhi kwa kitendo cha kumtolea ‘maneno ya shombo’ kocha wake, Jackson Mayanja.
    Isihaka, Nahodha Msaidizi wa Simba anadaiwa kumtolea maneno yasiyofaa kocha wake, Mganda Mayanja kabla ya mchezo dhidi ya SIngida United wa hatua ya 16 Bora Kombe la Shirikisho Tanzania (TFF), maarufu kama Kombe la Azam Sports Federation Jumapili.
    Lakini leo, Nahodha huyo Msaidizi ameomba radhi kwa mwalimu huyo, viongozi na wapenzi wa Simba SC, akisema kwamba anakiri kosa na hatarudia.
    “Sikuwa na lengo baya, kuna mambo nilitaka kujua kwa mwalimu kuhusu mimi, labda namna nilivyouliza haikumpendeza kocha, ndiyo maana ninaomba msamaha,”amesema Kessy.
    Hassan Isihaka ameomba radhi kwa kocha wa Simba SC, Jackson Mayanja

    Aidha, Kessy ameomba uongozi umsamehe na kumrudisha kundini, akiahidi kutorudia tena kufanya kitendo chochote chenye tafsiri ya utovu wa nidhamu.
    Pamoja na kusimamishwa kwa muda usiojulikana na uongozi wa klabu kufuatia kikao cha Kamati ya Utendaji, Isihaka pia atalipwa nusu ya mshahara kwa kipindi chote cha adhabu yake. 
    Mapema leo, kocha Mayanja amesema kuwa beki huyo alistahili adhabu kutokana na kufanya kitendo cha utovu wa nidhamu.
    Alisema kwamba anasikitika kuona nidhamu ya wachezaji inapungua na kuharibu vipaji vyao wakati timu na nchi zinawategemea nyota chipukizi.
    Mayanja alisema kwamba kila mchezaji Simba atapata nafasi ya kucheza kulingana na nafasi na aina ya mpinzani wanayekutana naye kwenye ligi au mashindano yoyote watakayoshiriki.
    Simba ipo kambini Morogoro tangu jana kujiandaa na mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Mbeya City mwishoni mwa wiki.
    "Tuko tayari Morogoro, timu itakuwa inafanya mazoezi mara moja kwa siku, ila kutakuwa na siku moja ambayo tutafanya mazoezi mara mbili, najua Mbeya City ni timu nzuri na yenye kuhitaji kushinda, haiko katika nafasi mbaya kulingana na changamoto za mechi zinavyoendelea," alisema Mayanja.
    Mbali na Isihaka, mchezaji mwingine wa kikosi cha kwanza ambaye hakwenda Morogoro juzi ni beki, Hassan Kessy ambaye anasumbuliwa na Malaria.
    Simba itaikaribisha Mbeya City ambayo sasa iko chini ya Mmalawi, Kinnah Phiri Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, ikihitaji ushindi lazima ili kufufua matumaini ya ubingwa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ISIHAKA AOMBA RADHI SIMBA, MAYANJA ASEMA ALISTAHILI ADHABU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top