• HABARI MPYA

    Monday, September 23, 2019

    YANGA SC WAONDOKA KESHO DAR KUIFUATA ZESCO UNITED MECHI YA MARUDIANO LIGI YA MABINGWA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KIKOSI cha Yanga kinatarajiwa kuondoka kesho mjini Dar es Salaam kwenda Zambia kwa ajili ya mchezo wa marudiano hatua ya mwisho ya mchujo wa kuwania kuingia hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya wenyeji, Zesco United Ijumaa Uwanja wa Levy Mwanawasa mjini Ndola.
    Yanga ambayo inaendelea na mazoezi Uwanja wa Chuo cha Maafisa wa Polisi, Kurasini mjini Dar es Salaam inatakiwa kushinda ugenini baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 nyumbani Septemba 14 Uwanja wa Taifa.
    Kocha wa Yanga SC, Mwinyi Zahera kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ana matumaini makubwa ya kurudia alichokifanya kwenye Raundi ya kwanza, alipoichapa Towsnhip Rollers 1-0 mjini Gaborone nchini Botswana baada ya sare ya 1-1 Dar es Salaam.

    Viungo Deus Kaseke (kulia) na Patrick Sibomana (kushoto) wamo kwenye kikosi cha Yanga SC kinachoondoka kesho kwenda Zambia

     Katika mchezo dhidi ya Zesco, Yanga SC walitangulia kwa bao la mkwaju wa penalti la kiungo wa kimataifa wa Rwanda, Patrick Sibomana dakika ya 24 akimchambua vizuri kipa wa kimataifa wa Zambia, Jacob Banda.
    Na Yanga walielekea kabisa kuondoka na ushindi kama makosa ya walinzi na kipa wao, Metacha Mnata kumruhusu kiungo wa zamani wa klabu hiyo, Mzimbabwe Thabani Kamusoko kuisawazishai Zesco kwa shuti la mbali dakika ya 90 na ushei.
    Mshindi wa jumla ataingia hatua ya makundi, wakati atakayefungwa ataangukia kwenye kapu la kuwania kucheza hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho. 
    Kikosi cha Yanga SC kinachotarajiwa kuondoka kesho ni makipa; Metacha Mnata na Farouk Shikalo.
    Mabeki; Juma Abdul, Ali Hamad, Muharami Issa ‘Marcelo’, Ally Mtoni ‘Sonso’, Lamine Moro, Kelvin Yondan, 
    Viungo; Raphael Daudi, Mapinduzi Balama, Feisal Salum, Mohammed Issa ‘Banka’, Mrisho Ngassa, Abdulaziz Makame, Papy Kabamba Tshishimbi, Sadney Urikhob, Patrick Sibomana, Juma Balinya, Deus Kaseke na Jaffar Mohamed na mshambuliaji pekee, Maybin Kalengo.
    Benchi la Ufundi ltaongozwa na Zahera, Msadizi wake, Mzambia Noel Mwandila, Kocha wa Makipa Manyika Peter, Mchua Misuli Jackob Onyango, Daktari Edward Bavu, Mratibu Hafidh Saleh na Mtunza Vifaa Mahmoud Omar ‘Mpogolo’.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC WAONDOKA KESHO DAR KUIFUATA ZESCO UNITED MECHI YA MARUDIANO LIGI YA MABINGWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top