• HABARI MPYA

    Thursday, October 12, 2017

    KICHUYA AAHIDI KUENDELEA KUFANYA MAKUBWA SIMBA SC

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    WINGA machachari, Shiza Ramadhani Kichuya ameahidi kuendelea kufanya vizuri ili kuisaidia klabu yake, Simba katika michezo ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inayoendelea.
    Kichuya ameyasema hayo leo kwenye mazoezi ya klabu hiyo Uwanja wa Boko Veterani mjini Dar es Salaam baada ya kukabidhiwa Medali za Mchezaji Bora wa Mechi mbili zilizopita za Simba dhidi ya Mbao FC Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza na Stand United Uwanja wa CCM Kambarage mjini Shinyanga. 
    Kichuya alifunga bao moja katika kila mchezo, Simba ikitoa sare ya 2-2 na Mbao na kushinda 2-1 dhidi ya Stand United na haikuwa ajabu alipopigiwa kura nyingi na wapenzi na wanachama wa klabu hiyo kuwa ‘Simba App Man of The Match’. 
    Shiza Kichuya (katikati) baada ya kukabidhiwa Medali zake leo Uwanja wa Chuo cha Maofisa wa Jeshi la Polisi, Kurasini mjini Dar es Salaam  

    “Ahadi yangu kwa kila ambaye ameona kipaji changu na jitihada zangu uwanjani na hatimaye kunipigia kura ni kuwa sitamwangusha, nitapambana kuhakikisha naendelea kufanya vizuri katika kila mchezo ambao nitapata nafasi ya kucheza,”amesema mchezaji huyo wa zamani wa Mtibwa Sugar ya Morogoro.
    Kichuya ameongeza kwamba Medali hizo zitakwenda kumpa nguvu nyingine ya kuhakikisha anaendelea kufanya vizuri ili kuendelea kuwa mchezaji muhimu ndani ya kikosi cha Wekundu wa Msimbazi.
    Simba SC inaendelea na mazoezi kujiandaa na mchezo wake ujao wa Ligi Kuu dhidi ya Mtibwa Sugar Jumapili Uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam.
    Ni mchezo ambao Simba inatarajiwa kumpiga kumbo mmoja wa washindani wake wawili hadi sasa kwenye mbio za ubingwa, Mtibwa Sugar – mwingine Azam FC ambaye Jumamosi atakuwa mgeni wa Mwadui FC mkoani Shinyanga. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KICHUYA AAHIDI KUENDELEA KUFANYA MAKUBWA SIMBA SC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top