• HABARI MPYA

    Monday, May 08, 2017

    SAMATTA AFUNGA GENK YASHINDA 2-1 KUWANIA TIKETI YA ULAYA

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta usiku wa jana amefunga bao la pili, timu yake, KRC Genk ikishinda 2-1 dhidi ya KAS Eupen Uwanja wa Luminus Arena, Genk kwenye mchezo wa Kundi B kuwania tiketi ya kucheza michuano ya UEFA Europa League mwakani.
    Samatta alianza katika mchezo huo na baada ya beki Mfinland, Jere Uronen kufunga bao la kwanza dakika ya 18, naye akafuatia kwa kufunga la pili dakika ya 28 akimaliza ukame wa mechi tano za kucheza bila kufunga.
    Mbwana Samatta akipiga hesabu za haraka za kumfunga kipa wa KAS Eupen, From Crombrugge 
    Tayari amemfunga na anaanza kukimbia kushangilia bao lake
    Hapa Mbwana Samatta anashangilia baada ya kufunga lake

    Kwa matokeo hayo, Genk inaendelea kuongoza Kundi B katika mchuano wa kuwania tiketi ya Europa League mwakani kwa kufikisha pointi 19 baada ya kucheza mechi saba na Samatta jana ameichezea Genk mechi ya 56 tangu ajiunge nayo Januari mwaka jana kutoka TP Mazembe ya DRC akiwa amefunga mabao 19 sasa.
    Kati ya mechi hizo 56, michezo 18 Samatta alicheza msimu uliopita na 38 msimu huu na kati ya hiyo, ni michezo 34 tu ndiyo alianza, 10 msimu uliopita na 24 msimu huu.
    Mechi 21 kati ya hizo alitokea benchi, nane msimu uliopita na 13 msimu huu, wakati 11 hakumaliza baada ya kutolewa, tano msimu uliopita na sita msimu huu na katika mabao hayo 19, 14 amefunga msimu huu na tano msimu uliopita.
    Kikosi cha Genk kilikuwa; Ryan, Uronen, Colley, Dewaest, Castagne, Berge, Malinovskyi, Authors/Nastic dk79 Boetius/Naranjo dk75, Buffalo/Walsh dk88 na Samatta.
    KAS Eupen: From Crombrugge, Diallo/Timmermans dk71, Diagne, Jeffren, Garcia, Bassey, Wague, Bruls, Onyekuru, Blonde Elle na George.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA AFUNGA GENK YASHINDA 2-1 KUWANIA TIKETI YA ULAYA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top