• HABARI MPYA

    Thursday, May 25, 2017

    NI GHANA NA MALI FAINALI U-17 AFRIKA, NIGER NA GUINEA NJE

    Na Mwandishi Wetu, LIBREVILLE
    KIPA Youssouf Koita usiku wa Jumatano alikuwa shujaa wa Mali baada ya kuwawezesha mabingwa hao watetezi kutinga fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa vijana chini ya umri wa miaka 17 kwa ushindi wa penalti 2-0 dhidi ya Guinea Uwanja wa l’Amitie mjini Libreville, Gabon.
    Mali sasa watakutana na Ghana katika fainali Jumapili baada ya timu hiyo nayo kuitoa Niger kwa penalti 6-5 kufuatia sare ya 0-0 kwenye Nusu Fainali nyingine Uwanja wa Port Gentil.
    Katika penalti, Le Syli Cadets walikosa mikwaju yao yote minne ikiwemo mitatu iliyookolewa na Koita, wakati wachezaji wenzake Hadji Drame na Fode Konate wakaifungia Mali na kuipeleka katika nafasi ya kurudia mafanikio yake ya Niamey miaka miwili iliyopita ilipoifunga Afrika Kusini 2-0 kwenye fainali.  
    Youssouf Koita ameokoa penalti tatu na kuiwezesha Mali kutinga fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa U-17 

    Jumapili, Mali itamenyana na Ghana kuwania Kombe wakati Guinea itamenyana na Niger katika mchezo wa kuwania nafasi ya tatu Uwanja wa l’Amitie mjini Libreville.
    Ikumbukwe Ghana imetokea Kundi A ambako ilikuwa na Guinea, Cameroon na wenyeji Gabon, wakati Mali imetokea Kundi B ambako ilikuwa na Niger, Tanzania na Angola. Zote, Ghana, Mali, Guinea na Niger zimefuzu fainali za Kombe la Dunia la U-17 nchini India Oktoba mwaka huu.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NI GHANA NA MALI FAINALI U-17 AFRIKA, NIGER NA GUINEA NJE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top