• HABARI MPYA

    Thursday, May 04, 2017

    JEMADARI SAID ‘AMFICHUA’ ADUI WA SOKA YA LINDI

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    WADAU na wapenzi wa soka mkoani Lindi wameshauriwa kuweka kando tofauti za itikadi za kisiasa na kuunganisha nguvu zao katika kuhakikisha mkoa huo unakuwa na timu katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara tena.
    Ushauri huo umetolewa na gwiji wa soka mkoani humo na mchezaji wa zamani wa timu marufu Lindi, Kariakoo United, Jemadari Said katika mahojiano maalum na Bin Zubeiry Sports – Online jana mjini Dar es Salaam.
    Jemadari ambaye kwa sasa ni Ofisa wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), amesema kwamba Lindi ilibahatika kuwa na timu moja imara katika Ligi Kuu kati ya 1999 na 2001, Kariakoo United lakini kwa sababu ya tofauti za itikadi za kisiasa ikateremka Daraja.
    Nyota wa zamani wa soka mkoani Lindi, Jemadari Said (kushoto) akiwa na Rais wa TFF, Jamal Malinzi 



    “Huu mpira wetu Lindi, kwangu mimi kwa ujumla ni siasa na mitazamo ya kiitikadi za vyama vya siasa imepelekea watu kushindwa kufikiria kwenye mambo yao ya kuendeleza mpira tukafikia hatua ambayo sasa Lindi hatuna cha kujivunia,”amesema.
    Mchezaji huyo wa zamani wa timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 20, amesema watu walikuwa wanaamini vigogo wa CCM mkoani humo waliokuwa wanaifadhili Kariakoo walikuwa wananufaika kisiasa wakaamua kuleta mgawanyiko uliosababisha kushuka kwa timu na baadaye kupotea kwenye ramani.
    Jemedari aliyekuwa mkali wa mabao katika Ligi Kuu enzi zake anacheza, alisema hata sasa itikadi na tofauti za kisiasa zinaendelea kuitafuna soka ya Lindi kiasi kwamba inashindikana kurejesha timu Ligi Kuu.
    Amesistiza ipo haja ya wana Lindi kuweka kando itikadi za kisiasa kwenye masuala ya michezo na kuunganisha nguvu zao kuhakikisha wana kuwa na timu katika Ligi Kuu tena.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: JEMADARI SAID ‘AMFICHUA’ ADUI WA SOKA YA LINDI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top