• HABARI MPYA

    Monday, September 19, 2016

    SIMBA YAUKATAA UWANJA WA UHURU, YATAKA KUREJEA TAIFA

    Na Mahija Kitwana, DAR ES SALAAM                      
    KLABU ya Simba SC imeomba kurejesha mechi zake za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Taifa kutoka wa Uhuru, Dar es Salaam ili kuwalinda wachezaji wake na maumivu.
    Katibu Mkuu wa Simba, Patrick Kahemele amesema kwamba wamemuandikia barua Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi, Boniphace Wambura kuomba kurejesha mechi zao Taifa baada ya kubaini Uwanja wa Uhuru haupo vizuri.
    Kahemele amesema kwamba wachezaji wao watatu waliumia katika mchezo uliopita wakishinda 1-0 dhidi yaAzam FC kutokana na ubaya wa eneo la kuchezea la Uwanja.
    Ibrahim Hajib wa Simba akipasua katikati ya wachezaji wa Azam FC Jumamosi Uwanja wa Uhuru

    “Vile vipira vya kwenye nyasi bandia pale uwanjani vimeharibika kutokana na kutotumika kwa muda mrefu, kwani vimepigwa jua, vimefubaa na kuwa kama vipande vya chupa, hivyo kuhatarisha usalama wa wachezaji wanapoanguka,”amesema Kahemele.
    Katibu huyo pia akasema Uwanja wa Uhuru ni mdogo ambao hauendani na mahitaji ya soka ya kisasa na kwamba hawatakuwa tayari kuutumia tena hadi hapo utakapokaguliwa na kuidhinishwa a wakaguzi wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF) na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA).
    “Hatutaki na hatutoutumia Uwanja wa Uhuru hadi pale utakapofanyiwa marekebisha makubwa na kukaguliwa na wakaguzi wa CAF na FIFA,”alisema Meneja huyo wa zamani wa Azam FC.
    Pamoja na kuulalamikia Uwanja wa Uhuru, Simba SC imeshinda mechi zake zote ilizocheza hapo dhidi ya Ruvu Shooting 2-1, Mtibwa Sugar 2-0 na Azam 2-0.
    Katika mechi zake mbili za awali ilizocheza Uwanja wa Taifa, ilishinda moja 3-1 dhidi ya Ndanda FC ya Mtwara na kutoa sare ya 0-0 na JKT Ruvu. 
    Baada ya barua hiyo, sasa linasubiriwa tamko la Bodi ya Ligi juu ya wapi mchezo ujao wa Simba SC dhidi ya Maji Maji ya Songea utachezwa.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA YAUKATAA UWANJA WA UHURU, YATAKA KUREJEA TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top