• HABARI MPYA

    Saturday, April 02, 2016

    YANGA KUMKOSA HARUNA KESHO DHIDI YA KAGERA

    YANGA SC itamkosa kiungo wake, Haruna Niyonzima (pichani kulia) kesho katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Kagera Sugar Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Nahodha huyo wa Rwanda anasumbuliwa na Malaria, hivyo hatakuwemo kabisa kwenye programu ya mechi mbili zijazo za Yanga.
    Baada ya mechi na Kagera Sugar kesho, Yanga watarudi dimbani kwenye Uwanja huo huo Jumamosi ijayo kumenyana na Al Ahly ya Misri katika Ligi ya Mabingwa ya Afrika.
    Na Niyonzima hatacheza mechi dhidi ya Ahly kwa sababu atakuwa anatumikia adhabu ya kadi mbili za njano alizopewa kwenye mechi mfululizo za Raundi ya Kwanza ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya APR ya kwao, Rwanda.
    Pamoja na kumkosa kiungo wa Amavubi kesho, habari njema ni kwamba Nahodha wa timu, beki Nadir Haroub 'Cannavaro' sasa yuko fiti kabisa kurejea uwanjani.
    Cannavaro alicheza kwa dakika tano za mwisho katika mchezo dhidi ya Ndanda FC Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Alhamisi Yanga ikishinda 2-1 baada ya kukosekana tangu Novemba mwaka jana alipoumia akiichezea timu ya taifa dhidi ya Algeria mjini Blida.     
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA KUMKOSA HARUNA KESHO DHIDI YA KAGERA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top