• HABARI MPYA

    Wednesday, March 02, 2016

    MAPUNDA APEWA KUCHEZESHA MECHI YANGA NA AZAM JUMAMOSI TAIFA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    REFA mkongwe nchini, Kennedy Mapunda atachezesha mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kati ya wapinzani wakuu wa mbio za ubingwa, Yanga na Azam.
    Miamba hiyo inamenyana Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam katika mchezo wa Ligi Kuu mzunguko wa pili, ikiwa inafungana kwa pointi 46 kila moja na idadi sawa ya mechi za kucheza, 19 kila timu.
    Na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limemteua refa huyo mwenye uzoefu kuaongoeza mchezo huo Jumamosi, akisaidiwa na Frank Komba na 
    Soud Lilla watakaoshika vibendera, wakati mezani atakuwa Elly Sasii.
    Beki wa Azam FC, Shomary Kapombe (kushoto) akibinuka tik tak kuokoa katika moja ya mechi zilizopita dhidi ya Yanga. Wengine kulia ni beki wa Yanga, Kevin Yondan na kipa wa Azam, Aishi Manula 

    Jumamosi utakuwa mchezo wa pili kuzikutanisha timu hizo mwaka huu, na ya tano kwa ujumla msimu huu tangu zilipokutana katika Kombe la Kagame Julai mwaka jana, kila timu ikishinda mara moja na nyingine zote kutoka sare.
    Julai 29, mwaka jana, timu ya Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa na familia yake iliifunga Yanga SC kwa penalti 5-3 katika Robo Fainali ya Kombe la Kagame kufuatia sare ya 0-0 ndani ya dakika 90.
    Agosti 22, mwaka huu, Yanga SC ikalipa kisasi baada ya kushinda kwa penalti 8-7 kufuatia sare ya 0-0 ndani ya dakika 90 katika mchezo wa Ngao ya Jamii kabla ya sare mbili mfululizo za 1-1, kwanza kwenye Ligi Kuu Oktoba 17, mwaka jana na baadaye kwenye Kombe la Mapinduzi Januari 5, mwaka huu.
    Oktoba 17, mwaka jana Yanga ndio walikuwa wa kwanza kupata goli dakika ya 45 kupitia kwa Mzimbabwe Donald Dombo Ngoma aliyepokea krosi ya Juma Abdul na kuwachambua mabeki wa Azam kisha kupachika mpira nyavuni – kabla ya Muivory Coast Kipre Tchetche aliyetokea benchi kipindi cha pili kwenda kuchukua nafasi ya Mkenya Allan Wanga kuifungia Azam bao la kusawazisha dakika ya 83 akimalizia pasi ya Farid Mussa.
    Katika mchezo huo, Yanga walipata penati baada ya kipa wa Azam Aishi Manula kumuangusha winga wa Yanga Simon Msuva kwenye eneo la hatari, kiungo Mzimbabwe Thabani Kamusoko akampelekea mikononi kipa wa Azam shuti lake.
    Na Januari 5, licha ya Azam FC kucheza pungufu baada ya Azam FC kumpoteza Nahodha wake, John Raphael Bocco ‘Adebayor’ aliyeonyeshwa kadi ya pili ya njano na refa Mfaume Ali Nassor dakika ya 62, lakini ikamudu kumaliza mechi kwa sare ya 1-1.
    Azam FC walitangulia kupata bao dakika ya 58 baada ya shambulizi la kushitukiza – sifa zimuendee mfungaji wa bao hilo, Kipre Herman Tchetche raia wa Ivory Coast aliyewakokota mabeki watatu wa Yanga SC hadi karibu kabisa na boksi na kufumua shuti lililompita kipa Deo Munishi ‘Dida’. Lakini beki Mtogo, Vincent Bossou aliisawazishia Yanga SC dakika ya 83 akimalizia mpira ulioparazwa kwa kichwa na Malimi Busungu baada ya kona ya Simon Msuva.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAPUNDA APEWA KUCHEZESHA MECHI YANGA NA AZAM JUMAMOSI TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top