• HABARI MPYA

    Saturday, October 14, 2017

    MWANJALI: SIMBA TUKO TAYARI KUWANYAMAZISHA MTIBWA KESHO

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    NAHODHA wa Simba SC, Method Mwanjali amesema kwamba wamejiandaa vizuri kwa mchezo wao wa kesho wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Mtibwa Sugar Uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam.
    Mwanjali amesema kwamba matarajio yao ni ushindi tu katika mchezo huo wa kesho, kwa sababu lengo lao ni kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu msimu huu.  
    Pamoja na hayo, Mwanjali amewataka mashabiki na wapenzi wa Simba kujitokeza kwa wingi kuisapoti timu yao katika mchezo wa kesho, ambao anatarajia utakuwa mgumu kama ilivyo kawaida kila timu hizo zinapokutana.
    Method Mwanjali amesema wamejiandaa vizuri kwa mchezo wao dhidi ya Mtibwa Sugar kesho

    “Tumejiandaa vyema na maandalizi ya kuelekea mchezo wetu wa Jumapili yanaendelea vizuri, mashabiki na wapenzi wote wa Simba wajitokeze kwa wingi kuja kutupa sapoti timu yao kwa ajili ya kupata matokeo mazuri,”alisema Mwanjali.
    Simba SC inaongoza Ligi Kuu kwa wastani wa mabao tu, ikiwa inalingana kwa pointi na zote, Azam FC na Mtibwa Sugar zenye pointi 11 kila mmoja na ushindi katika mchezo wa kesho utapunguza washindani kileleni. 
    Ligi Kuu inatarajiwa kuendelea leo na mabingwa watetezi, Yanga watakuwa wageni wa Kagera Sugar Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba, Mwadui FC wakiikaribisha Azam FC Uwanja wa Mwadui Complex, Shinyanga na Ndanda wakiwakaribisha jirani zao, Maji Maji ya Songea Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara wakati Singida United itasafiri hadi Uwanja wa Mabatini ulioko Mlandizi kucheza na wenyeji Ruvu Shooting ya Pwani.
    Majirani wengine, Njombe Mji na Lipuli ya Iringa watacheza kwenye Uwanja wa Sabasaba mjini Njombe ilihali michezo mingine ya Ligi hiyo ikifanyika Jumapili Oktoba 15, ambako Simba itakuwa mwenyeji wa Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam wakati Tanzania Prisons itacheza na Stand United kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MWANJALI: SIMBA TUKO TAYARI KUWANYAMAZISHA MTIBWA KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top