• HABARI MPYA

    Sunday, August 12, 2018

    MTIBWA SUGAR ‘RONYA RONYA’, YAKAMILISHA MECHI TATU IKIPIGWA ZOTE KABLA YA KUIVAA SIMBA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Mtibwa Sugar ya Morogoro leo imekamilisha mechi tatu za kujiandaa na msimu mpya bila ushindi, ikipoteza zote baada ya leo pia kufungwa 1-0 na Reha FC ya Temeke Uwanja wa Bandari, Tandika katika mchezo wa kusaka mshindi wa tatu wa michuano ya Kombe la Reha Day.
    Ikumbukwe, Mtibwa Sugar ambao ni mabingwa wa Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Azam Sports Federation Cup (ASFC), ilifungwa kwa penalti 4-3 baada ya sare ya 0-0 na timu ya Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, KMC  katika mchezo wa kwanza, hivyo kuangukia kwenye mechi ya kuwania nafasi ya tatu.
    Awali ya hapo, Mtibwa Sugar inayofundishwa wachezaji wake wa zamani, kocha Zubery Katwila anayesaidiwa na Patrick Mwangata chini ya Mkurugenzi wa Ufundi, Salum Mayanga ilifungwa 2-1 na Mbeya City Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.
    Matokeo haya yanamaanisha Mtibwa Sugar hawako vizuri kuelekea mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya mabingwa wa Ligi Kuu, Simba SC Agosti 18 mwaka huu Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.
    KMC iliyopanda Ligi Kuu msimu huu, imefanikiwa kutwaa ubingwa wa michuano hiyo baada ya ushindi wa 2-0 dhidi ya Transit Camp.
    Mabao ya KMC yamefungwa na Abdallah Masoud na Sameer Mohamed, hivyo kuashiria mwanzo mzuri wa msimu mpya kwa timu hiyo iliyopanda Ligi Kuu msimu huu na kukisuka upya kikosi chake chini ya aliyekuwa kocha wa Mbao FC ya Mwanza kwa misimu miwili iliyopita, Mrundi Ettienne Ndayiragijje.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MTIBWA SUGAR ‘RONYA RONYA’, YAKAMILISHA MECHI TATU IKIPIGWA ZOTE KABLA YA KUIVAA SIMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top